KUTUBU KWA AJILI YA DHAMBI ZA TAIFA
SEHEMU YA KWANZA
Paulo na Sila walipofika Beroya katika Matendo 17:10, tunaambiwa kwamba watu
wa Beroya walikuwa waungwana kuliko wale wa Thesalonike kwa sababu walilipokea
neno kwa utayari wote wa moyo na wakayachunguza maandiko kila siku waone kama
mambo yalikuwa ndivyo. Hakika hii ndiyo taratibu ambayo hupendekezwa na maandiko,
yaani kwamba kwanza tuone katika maandiko mafundisho yoyote mapya kabla ya kuyaamini
na kuyapokea mioyoni mwetu. Huku si kutoamini lakini inaonyesha kuwa tunapendezwa
na mambo kama hayo kama Mungu alivyoyafunua kupitia Neno lake. Tunatakiwa kuheshimu
na kumpenda Mungu kwa kuyafuata mambo yale ambayo ameyaonyesha kwetu kwa uwazi.
Hii pia ni ulinzi kwetu –tutalindwa toka madhara na udanganyifu kwa kulitunza
Neno lake kwa unyenyekevu.
Vivyo hivyo, kama tukimsikia mtu anahubiri na kutuambia tuamini hili au kufanya
lile, lakini hatuvioni vitu hivyo kufundishwa katika maandiko, basi tusipokee
mafundisho hayo kabisa. Haijalishi kama mafundisho yanatufikia kupitia msemaji
wa kimataifa anayetukuka, kitabu cha kikristo ambacho kimeuzwa nakala mamilioni
ulimwengu mzima, au mtu ambaye tunaweza kuwa tunamheshimu. Haijalishi hata kama
imetoka kwa Mtume au hata malaika kutoka mbinguni (Galatia 1:8), tusiamini wala
kupokea kama jambo hilo hatuwezi kuliona kwenye maandiko. Mtume Paulo alishangazwa
kwamba Wagalatia walikuwa wameiacha haraka namna hiyo Injili ambayo walikuwa
wameiamini na kuipokea, na kufuata mafundisho mengine ambayo yalikuwa mageni
kabisa na yaliyokuwa kinyume na kweli. Leo, pia tunaweza kushangazwa na jinsi
watu wa Mungu wanavyopokea mambo haraka na kirahisi rahisi, ambayo hayajafundishwa
katika Biblia. Hatuchunguzi biblia kuona kama mambo hayo yako hivyo.
Hakuna kitu kipya chini ya jua. Kama ilivyo katika nyakati za Agano Jipya, ndivyo
ilivyo leo kuna upinzani kati ya ukweli wa Injili na mafundisho ambayo yanataka
kututia katika kongwa la mawazo ya Agano la kale ambayo yamemalizwa katika Kristo.
Mafundisho haya si sehemu ya Agano jipya na wala hayamo kabisa. Watu hutumia
maandiko, hasa kutoka Agano la kale, na kuanza kuyajengea hoja. Mafundisho haya
hutuibia kweli, kama ilivyo katika Kristo Yesu na uhuru tulio nao katika yeye
(Gal.3:1, 5:1). Wanataka waturudishe katika mawazo ya Agano la kale ambayo yameondolewa
katika Kristo na mafanikio aliyoyapata Kalvari. Katika moyo wake na mwisho wake,
mafundisho haya yote huwakilisha mashambulizi juu ya kweli ya Injili ya Kristo
naye amesulibiwa. Huvuruga kweli ya Injili na kutupofusha tusiweze kuiona nguvu
ya kweli na utoshelevu wote wa mahubiri ya msalaba. Wanaoyainua sana mawazo
hayo hawana habari kama wanapingana na kweli, lakini bado mafundisho hayo si
sahihi na ya hatari. Paulo alipigana kwa nguvu kuwafungua watu wa Mungu toka
uongo kama huo na kuonyesha kuwa waalimu kama hao walisumbua kanisa na watabeba
hukumu kwa kufanya hivyo. (Galatia: 1:8,9; 5:10-12).
Sasa tufikirie juu ya wazo hili ambalo
limesifika sana siku hizi kwamba tunapashwa kutubu juu ya dhambi za nchi ambayo
tunaishi ndani yake. Kufuatana na fundisho hilo, Mungu huumizwa kwa sababu ya
uovu katika nchi “yetu”, na uovu unamzuia Mungu asibariki nchi na watu wake
kama ambavyo angependa. Na pia nchi inakuwa chini ya laana au hukumu. Kwa sababu
hiyo tunapashwa kuungama na kutubu kwa sababu ya maovu katika nchi yetu na kwa
sababu ya dhambi ambazo watu wanazifanya, ili kwamba Mungu asamehe uovu huu
na kutuma baraka zake - inabidi tupokee upatanisho kwa ajili ya nchi yetu na
watu wake. Wanaendelea kufundisha kwamba ni lazima pia kutubu kwa ajili ya dhambi
zilizofanywa na vizazi vilivyopita katika nchi yetu – dhambi za kitaifa kabla
Mungu hajaleta baraka kweli kweli au kuleta uamsho. Katika insha hii ninajaribu
kusema juu ya mafundisho haya. Lakini kadri mafundisho haya yanavyoendelea kuzunguka
ulimwenguni, dondoo zingine zinaimalishwa zaidi au kusisitizwa zaidi kuliko
nyingine, na yale ambayo watu huamini yanaweza kutofautiana kwa namna fulani.
Kwa hiyo katika insha hii si kwamba namjibu mwandishi mmoja tu bali jibu langu
ni kwa mawazo mbalimbali ambayo yameendelea na kupata sifa kati ya mengi ulimwenguni.
Kwangu binafsi, ninaamini kuwa mtu anaweza kwa haraka haraka na kirahisi kuonyesha
kwamba mawazo haya yako kinyume na maandiko, lakini kwa sababu watu wengine
wameshawishika kwa kina sana kwa mafundisho haya mbalimbali, nimegusia karibu
kila vifungu, kama si vyote ambavyo hutumiwa katika jaribio la kuunga mkono
mawazo yao, ili mtu asije akadhani kuwa mafundisho haya yana maana yoyote ya
kibiblia.
Sasa, watu wanaofundisha vitu hivi hawavileti vitu hivi kama mawazo yao au tafsiri
zao lakini husema kwamba vimefundishwa katika maandiko kwamba tunapaswa kuvifanya
vitu hivi. Hili ni jambo la kutisha. Ni mamlaka gani waliyonayo ya kuwabebesha
wakristo mzigo huo? Tutaona kwamba hawana mamlaka yoyote kufundisha vitu hivi.
Ni utunzi wao mpya kabisa. Ni udanganyifu unaotuondoa kutoka kwenye kweli na
nguvu ya msabala. Haimtukuzi Kristo na kazi yake ya Kalvari lakini matokeo yake
ni kuzitukuza baadhi ya sehemu za sheria na kwa njia hiyo kuwaleta watu wa Mungu
kwenye udanganyifu na kongwa. Haifundishwi hasa hata katika Agano la kale, ingawa
hapa ndipo wanapo kimbilia ili kuhalalisha mafundisho haya. Wanatafuta tukubaliane
na taswira za baadhi ya watu na Agano la kale kama Eliya, Yeremia, Yona au Daniel
(ingawa kuna vitu tunavyoweza kuvisifia juu yao), badala ya kutuletea mfano
wa ufunuo wa Yesu Kristo, ambaye yu juu ya hao wote, katika asili yake ya uungu
na pia huduma yake. Mafundisho haya yanataka kuturudisha katika namna ya Agano
la kale ya kufikiri juu ya laana na hukumu juu ya mataifa, badala ya kutambua,
kukiri na kuutangaza kutolewa kwa msamaha katika siku hizi za neema. Lakini
zaidi ya haya, wanaishia katika kuwatumbukiza watu katika mawazo na maombi ya
kishirikina, kwa kulielewa vibaya hata Agano la kale. Hii haina maana kwamba
tusiombe juu ya baadhi ya hali za kijamii ambazo zina athiri saana jamii zetu
au uenezaji wa Injili. Tutagusa juu ya jambo hili baadaye, lakini mawazo haya
ya kisasa yanaenezwa zaidi ya haya.
Swala ni rahisi tu, ni hili, kama vitu hivi vinahitajika na watu wa Mungu, yaani
kuungama au kutubu dhambi ambazo hutokea katika nchi yao, mji au sehemu, ili
kwamba hukumu ya Mungu au laana juu ya nchi iondolewe na baraka kuja, sasa kwa
nini jambo hili halifundishwi kaatika Agano Jipya? Kwa nini hakuna hata aya
moja ambayo inafundisha au kuelekeza tufanye jambo hili? Hata haikutajwa wala
kuashiriwa. Kumbuka, wanataka kutuambia kwamba baraka za kweli au uamsho katika
nchi yetu huzuiliwa kama hatuungami na kutubu kwa ajili ya dhambi za vizazi
vya sasa na vilivyopita! Ni kwa vipi jambo la maana kama hili kwa ajili ya maendeleo
na kuenea kwa Injili lisiwepo kabisa katika mafundisho ya Agano Jipya? Hakuna
kabisa katika Agano Jipya kitu ambacho kingetuongoza ingalau kufikiria vitu
kama hivyo. Tutaona pia jinsi ambavyo walimu hawa hulitafsiri visivyo Agano
la kale katika jaribio lao la kuhalalisha mafundisho haya.
Mitume Hawakutumia Mtazamo Huu
Fikiria matendo ya mitume. Ni wapi mtazamo huu ulikuwa mkakati wa mitume, wakifikiri
au kufundisha wasafiripo kuizunguka dunia wakihubiri Injili? Ni wapi wanawaelekeza
wakristo au watu wengine wowote watubu dhambi za nchi zao, mkoa au mji ili baraka
za Mungu zije. Tunasoma wapi kuwa wao wenyewe walifanya kitu kama hiki? Lakini
haya ndiyo tunaletewa katika mafundisho haya – kwamba wakristo waungame na kutubu
kwa ajili ya dhambi za ulimwengu, yaani kwa dhambi za wasioamini katika maeneo
yao, ikiwa ni pamoja na vizazi vilivyopita. Hakuna mahali popote katika matendo
ya mitume jambo hili linaonekana. Mitume na wengineo husafiri kama Mungu anavyowaongoza;
kuhubiri Habari Njema kwa watu kwamba wamesamehewa bure kwa dhambi zao zote
kupitia kifo na kufufuka kwa Yesu Kristo; watu huokolewa na makanisa kuanzishwa
na wakristo hupokea mafundisho. Lakini hakuna kuungama au kutubu kwa ajili ya
dhambi za nchi yoyote au eneo na wakristo (au mtu awaye yote!) kabla ya kuipeleka
Injili mahali pale kwa uwezo – bila shaka Mungu alibariki kazi na kuongeza watu
wengi katika Kanisa pasipo mafundisho haya – wala hapakuwa na mafundisho kama
haya yakitolewa na mitume kwa wakristo wafanye hivyo baada ya makanisa kuanzishwa
ili kazi ya Mungu kati yao istawi na kuenea. Ilienea na kukua kwa ajabu na kulikuwa
na uamsho, pasipo watu wa Mungu kujiweka katika nafasi ya wasioamini kati yao
na kutubu dhambi zao. Pia ilienea kuwa ajabu kwa neema ya Mungu pasipo wenye
dhambi kuambiwa watubu juu ya dhambi (zilizopita au za wakati huo) za miji yao
mikuu au nchi zao, kabla ya Mungu kuwabariki kweli kweli na kutenda kazi kati
yao kwa nguvu! Mahali popote, mtu yeyote aliambiwa atubu kwa ajili ya dhambi
zake! Jambo hili kwa kweli ndilo fundisho na pia mfano tunaoukuta katika Biblia
yote, kama ambavyo tutaona.
Vivyo hivyo, kumekuwa na uamsho mara kadha ulimwenguni kote na Injili imeenea
na kuwa na mizizi tangu nyakati za mitume hata leo pasipo watu wa Mungu kufanya
vitu hivi, kujua au kufundisha. Kwa hiyo nani anaweza kutuambia kwa nini mafundisho
haya yameonekana mara kuwa ya lazima kwa kanisa na kwa mafanikio na kuenea kwa
Injili katika siku hizi?
Mitume Hawakufundisha Juu ya Mtazamo Huu
Mafundisho haya huwezi kuyakuta mahali popote katika maandiko ya mitume katika
Agano Jipya. Kitu kama hicho hakitajwi hata kidogo. Je tunaweza kusema basi
kuwa palikuwa na dhambi pungufu, uchawi na kuabudu sanamu kupungufu katika nyakati
za Agano Jipya kuliko zilizopo sasa na kwamba kwa hiyo wakristo wa nyakati hizo
hawa kuhitaji mafundisho haya kama tunavyohitaji leo. Hii ni wazi si kweli.
Na simjui mtu yeyote ambaye anayesema jambo hili. Maandiko ya Agano Jipya pamoja
na kumbukumbu za kihistoria zinahakiki wazi na kwa msisitizo kwamba kulikuwa
na ufisadi mkuu na dhambi za kutisha, uchawi, kuabudu sanamu na ugandamizaji
katika nyakati za Agano Jipya. Kwa mfano, Mdo 8:9-11; 13:6-8; 17:16; 19: 18,19,23-28.
Tunafahamu pia toka kumbukumbu za kihistoria kwamba jiji la korintho lilikuwa
ni mahali pa uzinzi mwingi na hii inaweza kusaidia kutoa maelezo kwa nini kanisa
la Korintho lilihitaji mafundisho maalum na kukemea kwa mtume Paulo. Vita vingi
vilikuwa vimetokea katika eneo hili la ulimwengu na dhuruma nyingi zilikuwa
zimetokea. Kidokezo hiki ni kikubwa kwamba hakihitaji ufafanuzi zaidi.
Kwa hiyo kwa nini mitume hawa hawawaambii wakristo watubu kwa ajili ya dhambi
ambazo nchi zao na maeneo yao yalikuwa yametenda katika kizazi hicho ama vilivyopita?
Je nchi zilikuwa hazijatenda uonevu wowote au ugandamizaji? Bila shaka zilikuwa
zimetenda lakini hakuna mahali popote mitume waliwaelekeza watu wa Bwana waombe
au watubu kwa sababu ya dhambi za Athene au kwa sababu ya uchawi na uabdu sanamu
wa Efeso au kwa sababu ya uzinzi wa jiji la Korintho, au kwa sababu ya ugandamizaji
wa Rumi juu ya nchi zingine hasa Yudea. Hakuna mahali ambapo tutaona wakitia
mkazo au kuwashinikiza wakiristo waungame na kutubu kwa ajili ya dhambi za kitaifa
au za vizazi vilivyopita. Hawawaambii wayahudi kwamba lazima waungame na kutubu
kwa ajili ya dhambi za mababa zao katika mwili; wala hawawaambii waamini wa
Kirumi, Kigiriki au Waarabu au wakristo wa nchi nyingine yeyote au eneo lolote
watubu kwa ajili ya dhambi za zamani za nchi zao. Hakika wakristo mjini Rumi
walikuwa na sababu lukuki za kuungama dhambi za himaya ya Kirumi kama mafundisho
haya yangekuwa kweli! Lakini hawapewi maelezo kufanya hivyo. Hakuna aya hata
moja, mkazo hata mmoja kwa wakristo wafanye hivyo mahali popote katika Agano
Jipya. Kulikuwa na dhambi nyingi mno, kuabudu sanamu, uchawi na ugandamizaji
katika siku zao na katika vizazi vilivyopita, kiasi kwamba mitume walikuwa na
kila sababu na fursa ya kutosha kuwakazia wakristo waungame au kutubu kwa ajili
ya dhambi za wale waliokuwa wamewazunguka – lakini kamwe hawakufanya namna hiyo.
Kwa hiyo tena tunaachiwa swali: kama kutubu kwa ajili ya dhambi za wasioamini
katika maeneo yetu au nchi ilikuwa lazima kwa ajili ya “upatanisho” wa nchi
na kwa ajili ya kuenea ufalme wa Mungu kwa nini mitume hawatuelekezi kufanya
hivyo? Je wamepuuza kutufundisha kitu ambacho kanisa linahitaji kujua ili Injili
isitawi na kuenea? Je walikuwa wajinga wasioweza kujua mafundisho muhimu kama
hayo, kama ni mafundisho muhimu kweli? Kama kanisa limejengwa juu ya msingi
wa Kristo, mitume na manabii, Je waalimu hawa wa kisasa wanajua zaidi ya wao?
Bila shaka wasingesema hivyo na wasingetaka kuwa hivyo, lakini naweka swali
hili ili kuonyesha wazi upotofu mkuu wa mafundisho haya na hatari ambayo waalimu
hawa wanajiingiza ndani yake. Hawajengi juu ya Kristo. Wanajenga juu ya tafsiri
zao juu ya Agano la kale. Wanabadilisha imani katika kristo na dini ya ushirikina!
Yesu Hakufundisha Mtazamo Huu
Yesu mwana wa Mungu hakuwaelekeza wafuasi wake wafanye hivyo mahali popote katika Injili hata katika ufunuo. Yesu alikuja akihubiri habari njema za ufalme wa Mungu kwa watu na kuwaambia watubu – na si kuwaambia watubu kwa niaba ya wengine! Wala hakuwaambia waungame au kutubu kwa ajili ya dhambi za vizazi vilivyopita kama kwamba hivyo ilikuwa lazima kwa ajili yao wapokee msamaha kamili na baraka toka kwa Mungu. Hasha. Na tuelewe kuwa kwa ajili ya Kalvari, mtu yeyote atubuye dhambi zake, hugeuka kumwelekea Bwana na hufanyika mwana wa Mungu, dhambi zilizopita za mababa zake au za taifa haziwezi kuweka mpaka au kuzuilia baraka kamili za Mungu katika Kristo Yesu kwa mtu huyo. Kalvari ni kukatwa kikamilifu toka dhambi, hukumu, toka kuhukumiwa moyoni na toka Adamu wa kale, hii ni pamoja na maisha yetu ya nyuma na mababu zetu nyuma. Mungu Asifiwe! Watu wa Mungu hawako kwenye kongwa lolote kwa ajili ya dhambi za mababu kama wako katika kristo! Hakuna kitu kama hiki kimafundisho ya Yesu au mitume. Angalia 2 Kor 5:17. Mawazo haya hayako ama sawasawa na maneno au Roho wa Kristo. Neno la Mungu huja kwa watu wenyewe, moja kwa moja kuwashawishi juu ya dhambi zao na kuwaongoza katika toba. Marko 1:14,15; 2:17 (Anawataka wenye dhambi watubu, wala si watakatifu watubu kwa dhambi za wenye dhambi!).
Neno la Mungu sasa linakuja kwa mtu binafsi na mmoja mmoja kwa kila mtu likiwatia hatiani kwa dhambi zao wenyewe: Luka 13:1-5; Mdo 2:38, 3:19; 8:22; 17:30; 26:20. Ni kwa njia gani wake kwa waume husikia kuhukumiwa kwa ajili ya dhambi zao kutubu na kumgeukia Mungu kwa imani na kupokea msamaha wa dhambi? Ni kwa njia gani baraka hii na neema ya Mungu inaloijia mioyo yao! Huja kwa kusikia neno la Mungu linalokuja mioyoni mwao wenyewe! Rumi10:10–17. Ndiyo, Yesu huwaambia wanafunzi wake waombe – lakini si kwa ajili ya dhambi za wenye dhambi katika miji mikuu, lakini badala yake waombe Bwana wa Mavuno atume watenda kazi (kuhubiri juu ya ufalme wa Mungu ili wenye dhambi wenyewe wasikie neno la Mungu na kwa njia hiyo kuamini na kutubu). Pia anawafundisha waombe ufalme wa Mungu uje na kwa mapenzi yake yatimizwe hapa duniani kama huko mbinguni, na ili kwamba tusamehewe kama tunavyowasamehe wengine. Lakini hakuna mahali popote katika Agano Jipya na hakuna mahali popote katika Biblia tunapoambiwa kutubu kwa niaba ya wenye dhambi, au kuungama dhambi zao ili kufanya upatanisho au mapatano kwa ajili yao kitendo ambacho kitamfanya Mungu awabariki! Yesu anaweza kutambua hukumu juu ya Kapernaumu na anaweza kulia juu ya Yerusalemu kwa sababu walifanya mioyo yao migumu kwa neno la Mungu na hawakutubu, lakini hawaombi wafuasi wake waungame na kutubu kwa dhambi za watu hao. (Bila shaka mifano hii inahusiana na Israeli kuikosa au kuikataa fursa ya kumpokea masihi wao).
Pia ona kwamba katika Uf.2:8-11, Bwana hakulitaka kanisa katika jiji la Smirma liombe na kutubu kwa ajili ya maovu yaliyokuwa yakitendwa na baadhi ya watu wa Smirna ambao ni wa Sinagogi la shetani, ili kwamba msamaha wa Mungu na baraka zake zije kwenye eneo: nasema tena, hakuna mahali popote katika biblia watu wa Mungu wametakiwa kufanya hivyo.
Lakini watu wengine huenda hata mbali zaidi katika kufundisha kwao, kwa kuwaambia watu wa Mungu kwamba watubu kwa ajili ya dhambi za mji au nchi, kama uchawi, uzinzi na ulevi na kuungama kwamba wao watu wa Mungu wanahusishwa katika dhambi hizi na wamemtenda Mungu dhambi! Watakatifu huambiwa wahusike na dhambi za wasio amini kama kwamba dhambi hizo ni zao! Huambiwa basi watumie damu ya Yesu katika hali hiyo ili kuleta upatanisho na kuomba msamaha wa Mungu! Lakini damu ya Yesu hutumika kwa moyo uaminio. Huwezi kuitumia damu ya Yesu kupitia maombi kwa mwenye dhambi asiyetubu! Huu ni kama uchawi katika ukamili wake ambao hutafuta kuchukua nafasi ya kristo ambaye ndiye mpatanishi pekee kati ya Mungu na Mwanadamu. Yesu katika jumuisho na hitimisho amejihusisha na dhambi za ulimwengu wote pale Kalvari, kwa njia ambayo ameleta msamaha kwa wote wanaoamini Injili. Usitafute kuongeza katika kazi ya Mungu katika Kristo.
Bila shaka wanaamini kuwa wanafuata
mifano ya Agano la kale (na tutaona hayo baadaye kwa kirefu) lakini tayari tumekwisha
kuona wazi kwamba hakuna wazo kama hilo katika Agano Jipya (na hata katika Agano
la kale kama tutakavyo ona pia). Hakika sasa tunaweza kulia pamoja na Paulo
na kusema,
“Enyi wagalatia msio na akili, ni nani aliyewaloga, ninyi ambao Yesu Kristo
aliwekwa wazi mbele ya macho yenu yakuwa amesulubiwa?”
Na isitoshe, mafundisho haya yanafanana na ulozi, mwishowe watu huamini mambo
ambyo, sio tu yako kinyume na maandiko, bali pia kinyume na kufikiri ipasavyo.
Wanao ushawishi wa kiuchawi juu ya watu wa Mungu wanaoyafuata mafundisho haya
pasipo kuhakikisha kwenye Biblia. Mafundisho haya yanaonyesha yanakubalika kwa
watu wengi kwa sababu walimu wao hutumia maandiko yaliyochaguliwa kwa uangalifu
sana (lakini kama walivyofanya kati ya makanisa ya Galatia, hasa kutoka katika
agano la kale) ambayo pengine huonyesha tarajio la ukweli ambalo linalingana
na la wakati ule; lakini hapo huongezea mawazo yao katika hilo. Na hii ndiyo
hatari na hila ya makosa ya aina hii, huku inatajwa kwamba wanatumia maandiko,
lakini hapo hapo wakiyakataa maandiko mengine - hivyo hujitokeza ukweli - lakini
wanatafsiri vibaya mistari hiyo ya neno la Mungu, wakiweka maana yao wao wenyewe
juu yake na ndipo huishia kupata kitu fulani ambacho kwa uhakika ni mbali na
ukweli na hata huwa kinyume cha ukweli. Kwa kukataa ushuhuda wote na maandiko,
wakijenga mtindo wao wa mafundisho, ingawa huwa hawanzii na Biblia hata kidogo.
Wanadai kuwa wanao ufunuo maalum au huduma - hata mitume kutoka kwa Mungu. Wanaanza
na mawazo ya aina fulani yaliyo ya kwao ambayo wao hufikiri labda yanaweza kufanya
kazi na pia ni ya kibiblia na baada ya hapo, wanajaribu kuyatafutia mistari
ya neno la Mungu, mstari wowote ambao unaweza kuonyesha kuunga mkono mafundisho
yao. Na wanapogundua kuwa kumbe biblia haiwaungi mkono kwa dhahiri, wanaanza
kujisomea maana zao wenyewe katika mistari hiyo waliyoichagua. Na wengi wamedanganyika
kwa njia hii, kwa sababu hawayachunguzi maandiko, wamesahau ile thamani ya usafi
na wepesi wa Injili ulivyotolewa kwao toka mwanzo.
Agano la Kale - Kwa Ujumla
Sasa, hebu tufikirie juu ya maandiko ya Agano la Kale, ambayo kwa hakika ni neno la Mungu lenye uvuvio kwetu. Ndani yake tunagundua mambo ya utendaji wa Mungu kwa wanadamu na hasa kwa watu wake aliowachagua, Israel, na maagano aliyoyaanzisha pamoja nao. Zaidi ya yote anatupatia picha ya mambo yanayokwenda kutokea hapo baadae na kutupatia mfano wa ufufuo wa wokovu ambao Mungu anakwenda kuuleta kwa wanadamu kupitia Yesu Kristo.
Ingawaje maandiko ya Agano la Kale yana mifano mingi inayomwonyesha Yesu katika namna yake na wokovu atakao uleta - matarajio ya mwenendo wa maisha ya Yusufu yanamdhihirisha Yesu k.m.f. Musa akiongoza wana wa Israel kupitia bahari ya Shamu ni picha ya ubatizo wetu katika Kristo. Lakini ili alisimamishe Agano Jipya na kuwaingiza waume na wake ndani ya ufalme wa kiroho wa Mungu, kwa hakika Mungu alipaswa kumleta Kristo mwenyewe na kumtuma afe katika msalaba. Kabla Kristo hajaziondoa dhambi za ulimwengu pale Kalvari (Yoh. 1:20), Mungu asingeleta au kuzaa chochote katika maisha ya ndani ya kiroho na uweza wa maisha yake yeye mwenyewe na ufalme. Agano la Kale linatupatia picha ya nje ya yale ambayo Mungu alipenda kutufanyia kiroho. Kwa kweli kifo cha Yesu pale Kalvari, kilikuwa ni kielelezo muhimu cha tukio la kihistoria ikiwa sio la umilele. Kifo chake kilibadilisha mambo kwa njia ya msingi kabisa. Alilia, “Imekwisha!”, na papo hapo pazia la hekalu likapasuka vipande viwili. Hii inaonyesha kuwa, watu kwa imani kupitia Kristo, sasa wangeweza kuingia patakatifu pa patakatifu kwa damu ya Yesu; katika roho; pasipo matendo ya sheria tena. Sheria ilitolewa na Musa, lakini neema na kweli zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo. Mungu habadiliki. Hata kidogo! Rehema zake kwa ajabu kabisa zinaonyeshwa kwa matendo yake na watu katika Agano la kale. Halikadhalika, haki yake na hukumu. Lakini sasa kwa sababu ya kifo cha Yesu pale Kalvari, uhusiano wa Mungu na wanadamu umepitia katika msingi wa mabadiliko makubwa. Yesu alikuwa ni mwanakondoo wa Mungu azichukuaye dhambi za ulimwengu, aliihukumu dhambi katika mwili wake hivyo kuivunja nguvu yake ndani ya maisha ya watu, alizichukua hukumu za dhambi za wanadamu, kwa hiyo akatupatia msamaha bure, akatupatia uzima, uzima wa milele kwa roho na haki yake (Rumi 8:1-4). Kwa ajili ya msalaba Mungu ameweza kufanya yale ambayo sheria isingeweza kufanya, na amewapa wale wanaoamini katika Kristo haki ya kufanywa kuwa wana wa Mungu na kuingia katika uwepo wake.
Kwa hiyo kati ya mambo mengine, mawili
ya msingi na muhimu yamebadilika. Kile ambacho Mungu amekifanya kwa ajili yetu,
ni kile ambacho Mungu amekifanya ndani yetu. Katika hii ya mwanzo, watu sasa
wanashiriki haki ya Mungu kwa imani, kwa sababu ya utajiri wa neema yake na
sio kwa kazi zipatikanazo kwa sheria, na hii inatupatia sisi haki ya kufanyika
kuwa wana wa Mungu.
Na kwa sababu Mungu amekwisha kutuondolea vyote viwili, dhambi na uadui wa sheria
(Efeso 2:15; Kol. 2:14), sasa kunakuwa na muungano wa kweli kiroho kati ya Mungu
na wanadamu. Hutufanya sisi tuwe watoto wake kwa kutupatia roho wa mwana wake
Yesu Kristo akaaye ndani yetu. Kutokana na hali hiyo basi, sasa maisha yetu
yanaonyesha tabia yake kwa njia ambayo haikuwezekana katika Agano la Kale (2
Petro 1:3-4). Kwa hiyo, iwapo tutarudia ili kuzitunza baadhi ya sehemu ya sheria
kama walivyofanya kule Galatia, hivyo basi, tutakuwa tunaikataa imani yetu katika
Kristo na wokovu wake aliotununulia, au kama tutakuwa tunarudi kuzifuata njia
za tabia za kale, ndipo basi tutakuwa tunakataa ufunuo wa tabia yake ndani ya
mioyo yetu.
Kwa mfano, katika Agano la Kale watoto wa kiume walilazimika kutahiriwa, kama
ni sehemu ya agano kati ya Mungu na watu wake. Hii ni aina au picha ya ndani
ya kazi za kiroho ambazo Kristo alizikamilisha kwa wale ambao wanamwamini yeye,
(Kol. 2:11). Lakini yeye ni utoshelevu wa kweli ambao kutahiriwa kwa nje katika
agano la kale ilikuwa inaelezea (Heb.10:1). Kwa hiyo, mtu yeyote kwa sasa, iwapo
anaamini kuwa pamoja na kuamini katika Kristo, ni lazima pia kwa nje utahiriwe
ili kuokoka, basi mtu wa jinsi hiyo atakuwa anaiondoa imani yake na wokovu aliopewa
(Gal. 5:3-6).
Ni ujinga ulioje jamani kuacha kitu muhimu na kubakia na kivuli chake! (Heb.10:1).
Je, unaweza kula kivuli cha tunda la ndizi? Kivuli kinaweza kukushibisha njaa
yako na kukuacha hai? Ebu - jaribu kula kivuli kwa kadiri uwezavyo. Lakini utaishia
na vumbi mdomoni mwako! Na jambo hili linafanana na mafundisho ya aina hiyo
yanavyofanya. Wanayaacha ya kiroho na kung’ang’ania ya kimwili, ya mbinguni
na wanang’ang’ania ya duniani, ingawaje mtu anaamini kuwa Yesu ni mwana wa Mungu
na kwamba anao msamaha kupitia damu yake; ingawa anaamini mambo mengineyo mengi
yaliyo ya kweli, bado mtu huyo, ikiwa anatafuta kuongezea chochote kwa yale
Kristo aliyoyafanya, iwapo anatafuta kuturudisha nyuma kwenye vitu ambavyo kwa
kweli Kristo alikuja kuviondosha au kutimiliza, hapo basi mtu huyo anasababisha
kuukataa wokovu wa Kristo. Kristo, na imani katika Kristo havina faida yoyote
kwake mtu huyo na hivyo imani ya mtu huyo ni bure. (Gal.4:19,20; 5:3,4). Hata
kama anajifikiria kuwa anamfuata Kristo, amejidanganya, (Gal. 3:1). Mtu wa jinsi
hiyo kwa jumla, anachanganya agano la kale na jipya, wanachanganya yale ya ndani
na ya nje; kivuli na kitu halisi, ya mwilini na ya rohoni ya duniani na ya mbinguni.
Inafanana pia kama Mkristo anafikiri ni lazima kutunza sherehe za Agano la kale.
Anaikataa Imani!
Kwa mtazamo wa yote ambayo Mungu ameyafanya kwa ajili yetu kwa Kristo Yesu,
haikushangaza kuona Mtume Paulo akihuzunishwa kutoka ndani ya moyo wake, akijitahidi
kadiri alivyoweza kwa maombi na maelekezo ili kuwakomboa Wagalatia kutokana
na ujinga wao wa madanganyo.
Je, unapaka damu leo katika miimo ya milango yako ili kuzuia hukumu ya Mungu?
Unaleta ng’ombe au mbuzi au kondoo pamoja nawe kanisani ili kumtolea Mungu kama
dhabihu ya dhambi zako? Haya, pengine labda unatabasam, kama mwitikio kwa maswali
haya! Lakini makosa ya jinsi hiyo hiyo yanafundishwa na kujitokeza siku za leo;
watu wanatafuta kuturudisha nyuma kwenye fikra, na matendo ya agano la kale.
Na wengi wa watu wa Mungu wanapokea na kuyafuata mafundisho hayo. Sasa, mafundisho
tunayoyaona ndani ya makala hii yanahusiana na aina hii ya makosa.
Niliyoyaelezea hapo juu ni mambo ya msingi ambayo Mungu amefanya kwa ajili yetu
katika Kristo - ambaye ndiyo njia ya wokovu wetu. Sasa vipi kuhusu huduma na
tabia ya Wakristo - Mungu anafanya nini ndani yetu na kupitia kwetu. Je, mambo
yanaendelea katika Agano jipya kama ilivyokuwa katika agano la kale? Kwa kiasi
tu. Lakini lazima tukiri juu ya mzizi wa mabadiliko ya msingi kwa sababu ya
Kristo na yale aliyoyafanya. Hebu fikiria Matayo 5: n.k. Sasa je, utambomoa
mwenzako jino lake, kwa sababu eti yeye amelibomoa lako? Je, utawachinja watu
wasioamini kwa upanga? Kanisa lako litampiga kwa mawe yeyote ambaye amefumaniwa
katika uzinzi? Au utamwita Mungu atume moto toka mbinguni uwajilie hao wanaompinga
Mungu? Haya yote yaliruhusiwa na kutakiwa ndani ya agano la kale. Lakini kwa
sasa hatuwezi; hatuwezi kuthubutu kufanya lolote kati ya hayo. Kwa sababu sisi
tumezaliwa upya kwa roho wa Mungu na wala hakuna kati ya hayo yanayofanana na
tabia yake Yesu ndani yetu.
Tunaweza kufikiri kwamba, haya yote ni rahisi na yaliyowazi kabisa, lakini ebu
umchukulie Yakobo na Yohana ambao kwa uwazi kabisa walipenda harufu ya uweza
wa kuwa na Yesu aliowapa. Hata hivyo walimwomba iwapo, angeweza kuita ili kushusha
moto chini, juu ya wasamaria kwa sababu wamekataa kumpokea Yesu. Aliwakemea
mara moja, na akawaambia, hawajui ni roho ya aina gani walinayo. Wao hawakuelewa
yote mawili, kati ya tabia na huduma ya mwana wa Mungu.
Na mpaka pale tu tutakapokuwa tunatembea katika Roho ya Kristo kufuatana na
neno lake, bado tutakuwa tu tukifanya makosa hayo hayo. Na hivyo ndivyo ilivyo
leo watu hawaelewi tabia ya Kristo na wokovu wake kadhalika na huduma ya kanisa.
Kutokana na uchaguzi wao kutafuta tabia ya ubinafsi wa madaraka, baadhi ya walimu
wao wamechagua maandiko kutoka katika Agano la Kale kwa kadiri yanavyowafaa
wao na vile wanavyotaka kuamini. Wanaumba mfano wa Mungu unaochipua toka katika
fikra zao, ambazo huzichochea baadhi ya nyaraka za Agano la Kale. Huu ni sawasawa
na kuabudu sanamu na hunyan’ganya mfano halisi wa Mungu kama ulivyofunuliwa
kwetu na katika Kristo.
Kwa hiyo, hii inatokana na watu hawa ambao huja mjini, na badala ya kuhubiri
Injili na utajiri usiochunguzika wa Yesu Kristo, wanawaambia watu kwamba eti
laana na hukumu za Mungu ni juu yao na miji yao na kwamba sasa wanatakiwa kutubu
kwa niaba ya dhambi za (wengine katika) miji hiyo au taifa hilo; ili kwamba
Mungu aweze kughairi na kuindoa hukumu yake na badala yake atume baraka (watu
wengine karibu wapumue moto na hukumu kama Yakobo na Yohana walivyotaka kufanya).
Tunawezaje kujua kuwa tumekwisha kuomba kwa ajili ya dhambi zote zinazotakiwa
kuungamwa? Lakini jee, watu wataendelea kutubu kwa jinsi hiyo hadi lini? Nani
atakaye waambia kwamba hukumu na laana hiyo sasa imeondolewa kwa toba ya jinsi
hiyo? Wahubiri hawa hawaonyeshi kabisa kuwaambia watu bali wanawataka tu wakristo
waaendelee kutubu na kutubu na kutubu kwa ajili ya mambo ya aina zote ambayo
hao wahubiri na wapelelezi wao pamoja na waombezi wao huendelea wakitafuta makosa
katika taifa!
Kwa kawaida, wanafurahishwa sana na ushahidi wowote ule juu ya mambo yahusuyo
siri za ulozi au uchawi katika nchi hiyo. Na kisha hutangaza waliyoyagundua
ndani ya makala zao na barua za maombi kwa maelezo makubwa. Wanazingatia sana
katika mambo ya aina hiyo na huzijaza akili za watu wa Mungu kwa masomo yasiyofaa
ambayo huelekea kwenye kutukuza kazi za shetani, badala ya kuiendeleza Injili
ya Bwana Yesu au kuleta baraka. Hayo ni madhara makubwa yanayowaingiza watu
katika ujinga wa kutomjua Kristo na wokovu wake wa tabia na huduma yake.
Tafadhali usielewe vibaya, hapa sisemi kuwa hatuwezi kuomba kuhusu mambo yatokezayo
katika miji au nchi zetu bali ninachosema ni kwamba tusifanye mambo ambayo hayamo
katika maandiko ya neno la Mungu; na tusiwe na mawazo ya ushirikina ambayo kwa
hayo watu wengine huyachanganya na Injili ya kweli hata kuwatumbukiza watu katika
vifungo na giza kwa mafundisho yao hayo. Katika siku hizi, kwa hakika tunaweza
kuumizwa kwa yale yanayotutokea pia yanayotokea katika kanisa, na tungependa
kunyenyekea mbele za Mungu na kuomba kuwa anaweza kugeuza mioyo ili imgeukie
na kuwaongoza watu kuelekea toba. Lakini hii inatofautiana sana na aini hii
ya maombi ya Ushirikina.
Agano la Kale - Daniel
Lakini sasa, kwa kadiri tunavyo yatazama maandiko ya Agano la Kale, kwa uhakika
tunagundua kwamba kumbe mafundisho ya jinsi hiyo hata hayamo humo!
Wapi katika Agano la kale ambapo Mungu au hata manabii anawainua watu wake ili
kuungama na kutubu kwa ajili ya dhambi ya yeyote yule asiyeamini au taifa lolote?
Au ni wapi tunaweza kuupata mfano wa jinsi hii katika Agano la Kale? Haupo wowote;
haupo; haupo hata mmoja.
Daniel ambaye hunukuliwa mara nyingi, alikuwa akiishi Babel, lakini pia huko
nako hatumkuti akiomba kwa ajili ya maovu ya mji ule. Hakuna popote ndani ya
Agano la Kale ambapo watu wa Mungu wanatubu kwa ajili ya dhambi za wasiomini,
ili kwamba laana ya Mungu ipate kuondolewa, na badala yake baraka na msamaha
upate kutolewa? Kwa kweli, hakuna yeyote aliyetubu kwa ajili ya dhambi za mtu
mwingine katika Biblia. Tunaona mifano ya watu wa Mungu wakiungama dhambi za
vizazi vilivyowatangulia – lakini hiyo ilitokea tu wakati ule Waisraeli walipopelekwa
uhamishoni na jambo hilo lilifanyika kwa niaba ya watu wa Mungu, na kamwe sio
kwa ajili ya wasioamini.
Je, Mungu amewatoa watu wengine au mataifa mengine kutoka katika baraka zake?
Hapana, ndani ya Agano la Kale tunayakuta yaleyale kama yalivyo katika agano
jipya. Mungu hulituma neno lake kwa watu wenyewe na huwainua ili kutubu juu
ya dhambi zao wao wenyewe. Wao wenyewe binafsi ndio wanaopaswa kutubu dhambi
zao, ndipo Mungu hujionyesha yeye mwenyewe kuwa yeye ni Mungu mwenye Neema isiyo
na ukomo na fadhili zake na baraka zake hufuatia mara moja! Lakini ikiwa ni
watu wenye kujaa majivuno na kufanya uovu ndipo hujulikana kuwa hukumu inawangojea
watu hao. Au ni kwa kupitia imani, ushuhuda, upendo na utiifu wa watu wa Mungu
katika Agano la Kale, ndipo watu huona kuwa jina la Bwana linatukuzwa katikati
ya mataifa na hivyo ndipo wengine hujiunga wenyewe pamoja na watu wa Mungu,
au huja kumwamini. Lakini wazo ya kwamba eti watu wa Mungu wanahitajika kuungama
na kutubu kwa ajili ya dhambi za mataifa yasiyoamini hivyo ndivyo iwe kama utangulizi
kwa Mungu ili aweze kubariki watu hao au taifa hilo, huo ni udanganyifu na ni
mambo ya kubuni ya kibinadamu na wala hayapatikani katika maagano yote mawili
ya kale na jipya. Sio hivyo tu bali hata wazo la aina hii linaweza kunyang’anya
wokovu wa bure alioununua Yesu Kristo pale Kalvari kwa ajili ya wanadamu. Mahala
ambapo alifananishwa na dhambi zao kiasi kwamba, dhambi zao zikawekwa juu yake
na akazichukua pamoja akafanywa dhambi, ili kwamba tufanywe wenye haki kwa Mungu
katika yeye. (Joh. 1:29; Rum.5:8-10; 2 Wakorinto 5:19-21; 1 Joh. 2:2.). Na hii
ndio sababu, katika siku hizi za Neema, Habari Njema inapaswa ihubiriwe kwa
watu wote, bure. Tumeambiwa katika sura hii kwamba, tulipokuwa tungali wenye
dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu, na kwamba tulipokuwa bado ni maadui,
tukapatanishwa na Mungu, kutokana na kifo cha mwanae. Haya ni maneno ya ajabu
ya wokovu wetu wa bure, ambapo Mungu alipoanzisha hatua ya kwanza, na akazishughulikia
dhambi zetu zote (wakati tulipokuwa tungali ni wenye dhambi), hata kabla hatujazijali
au kuzitambua. Sasa kwa nini basi tunahimizwa kutubu kwa ajili ya dhambi hizi
za watu wasioamini ambazo kwazo Kristo alishawafia? Kristo alizichukua dhambi
zetu zote ili kwamba kulingana na mtazamo wa Mungu, haliwi tena ni kizuizi kwake
katika kutupatia wokovu na uzima wa milele. Kwa hiyo inasemwa kwamba Mungu katika
Kristo hakutuhesabia dhambi yetu! Hayo yote ni kwa sababu ya Kalvari, na sasa
ni juu ya watu wenyewe kuiamini Injili na kutubu ili kwamba waweze kujua na
kupokea neema hii ya ajabu ya Mungu. Mungu amekwisha kufanya kila kitu kwa upande
wake - kwa jinsi ya ajabu na kwa fadhili zake; sehemu yetu sasa ni kuiamini
Injili na kutubu kwa ajili ya dhambi zetu binafsi na kuutafuta msamaha wa bure
katika na kupitia Kristo. Sehemu yetu sio kuzifufua dhambi za watu wengine ambazo
Kristo amezifilia na tayari amekwisha kupokea upatanisho ili kusudi tuweze kutubu
kwa ajili ya hizo na kupokea upatanisho tena! Kwa kufanya hivyo tutakuwa tumembadilisha
Kristo pamoja na kifo chake kwa maombi yetu ya kutubu kwa ajili ya Taifa!
Au, watu hawa wanatutaka tuamini kwamba Yesu alikufa kwa ajili ya dhambi za
ulimwengu mzima, kwa kila roho ndani yake, bali kwamba kifo chake pale Kalvari
hakijatosha kiasi na kile wanachokiita “ushiriki wa dhambi kitaifa”!? Kwa maneno
mengine hapo wanataka kusema - Kalvari haitoshi kiasi kwamba ni lazima tutake
hii nyongeza maalum “maombi ya upatanisho” ya kanisa ili kukileta kile wanachokiita
wao “suluhisho kwa taifa” ambalo Yesu hakuweza kumaliza pale msalabani! Kama
hivyo ndivyo ilivyo, basi tunaona kuwa kuingiliwa kwao kwa ubunifu wao unawalazimisha
zaidi kuingia ndani kabisa ya makosa na udanganyifu. Ni kama ilivyo katika kanisa
la Wagalatia - hawasemi kuwa ni Yesu tu, yeye pekee kasulibiwa kwa wokovu wetu;
bali wanasema, “Yesu pamoja na kutahiriwa kwa ajili ya wokovu.” Kwa hivyo mafundisho
hayo yanasema, “Yesu pamoja na kushirikisha kwa maungamo na toba” ili kuleta
wokovu kwa watu. Kwa hiyo wamezua wokovu katika hatua mbili - wanasema, ndiyo
Kalvari kwa hakika ni lazima lakini pia unahitaji toba ya upatanisho ili kusababisha
suluhu ya kitaifa na Mungu, kabla watu hawajapokea faida halisi ya Kalvari.
Hili ni kosa kubwa sana.
Na iwapo bado, wanasema kwamba maungamo na toba ya dhambi za taifa ya aina hii
kwa hakika hayamsababishi Mungu kusamehe taifa na dhambi zake, bali kwamba inafungua
tu njia ya Injili hii ya neema ili kuwabariki watu. Bado huo nao ni udanganyifu
mtupu, kwani aina hii ya maungamo na toba wala haifundishwi kabisa katika maandiko
ya neno la Mungu. Inaharibu tu ukweli uweza na wepesi wa Injili ndani ya akili
za watakatifu na wenye dhambi wote pia; inasababisha kuchanganyikiwa na ushirikina
ndani ya nchi.
Lakini wengine wa waandishi wao wanasema kuwa maungamo ya dhambi za kitaifa,
na kuomba msamaha, ina maana kwamba, shetani hawezi tena kuwashitaki watu hao
na kwa hiyo hawezi kuwaweka nje ya neema ya Mungu au kuwazuia kusikiliza Injili!
Kwa hakika ikiwa unaweza kusadiki hivyo, basi unaweza pia kuamini chochote kile!
Ni nini? Je, shetani anayo haki ya kuiweka nchi nje ya neema ya Mungu na kuwazuia
kusikiliza Injili mpaka hapo kanisa litakapoungama dhambi za taifa na kutafuta
suluhisho kwa ajili ya dhambi hizo? Hili ni kosa lenye ubaya uliokithiri; hivi
kweli hawa walimu hawajawahi kusikia juu ya Kalvari, na uweza wake! Kwa sababu
ya Kalvari, Mungu hawahesabii watu makosa yao, bali ametia ndani yetu neno la
upatanisho (2 Kor. 5:19). Amefungua mlango wazi! Yesu amefanya njia Kalvari
na shetani hana haki ya kuiweka roho nje ya neema ya Mungu, isipokuwa roho hiyo
yenyewe iasi neno la Mungu.
Ni wapi katika Agano jipya ambapo pameonyesha au kufundisha kwamba kanisa linahitaji
kuungama dhambi za mikoa ili lipate suluhisho kwa ajili ya dhambi hizo kabla
Mungu hajawabariki kwa neno la wokovu? Jambo hili linakaribia sana ya kuwa kufuru!
Kwa sababu ya kifo chake Kalvari, Yesu anayo haki kuwabariki na kuwaokoa watu
sawasawa na kusudi lake na kadiri ya neema yake!
Sasa tukifuatilia jambo hilo kwa undani zaidi, wanatuambia kuwa eti kwa sababu
Daniel aliziungama dhambi za taifa lake (Daniel 9), kwa hiyo basi, sisi nasi
tunahitaji kuungama na kutubu kwa ajili ya dhambi za taifa “letu” - hii ni kwamba
kwa ajili ya taifa lile tunaloishi, na kwa mji ule unaotuhusu.
Hakuna chochote kile kinachoonyesha kwa uwazi zaidi, kwa jinsi gani watu hawa
wanaofundisha hivyo hata wanavyochanganya mambo ya kimwili na ya kiroho; ulimwengu
na kanisa. Namna wanavyosoma ndani ya maandiko ni mawazo yao, na wala kwa kweli;
hawajali kuona kuwa Biblia inafundisha nini juu ya jambo hilo. Ndiyo, Danieli
alikuwa ni Mwisrael, akiomba kwa ajili ya taifa la Israel. Lakini katika Agano
la kale Israel ni watu wa Mungu, na wanawakilisha kanisa. Na Daniel alikuwa
ni mtu wa Mungu alikuwa akiwaombea watu wa Mungu (kanisa). Na maombezi yake
yanahusika na agano kati ya Mungu na watu wake na namna ambavyo watu wa Mungu
walilivunja Agano hilo na kupoteza urithi wao. Inafanana na jinsi ambavyo watu
hao wanavyonukuu mistari ya Biblia kama ile Ezekiel 22:30, na wanatuambia kwamba,
hii sasa inahusisha huduma ya kanisa katika kuomba kwa ajili ya dhambi za nchi
tunamoishi. Lakini tena mstari huo huo wa Biblia unamweleza Mungu, akitafuta
mtu kati ya watu wake aombaye, ameumizwa kwa ajili ya hali ya watu wa Mungu
(kanisa) na yeye ambaye anajali vyakutosha kuhusu heshima na utukufu wa Mungu
ili aweze kuomba mbele za Mungu kutokana na hali mbaya ya watu wake Mungu ambao
kwao aliwatengenezea agano (mapatano).
Lakini, ili waweze kuyahalalisha mafundisho yao, watu hao wanaitumia vibaya
mistari hiyo ya Biblia, wakiyabadilisha maombi yao kutoka kanisa (ambalo ni
watu wa Mungu waliokombolewa kwa agano na yeye) kwa ulimwengu, kama vile hivyo
ndivyo ilivyo au ingeweza kuwa sasa!
Ingawaje tunaweza au kutakiwa kuomba kwa ajili ya jamii tunayoishi, (kama vile
1Timotheo 2:1,2) -tutaliangalia hilo hapo baadae - katika mafundisho haya, na
kile tunachopaswa kukifanya, hakina msingi wa kibiblia. Hawaupati mfano wote
wa mafundisho haya ndani ya agano jipya; na kwa hiyo, wanamnukuu kwa wingi sana
kutoka katika Agano la Kale - lakini baadae tu huishia katika kushindwa katika
kuitumia mistari hiyo, na kwa ujumla kulichanganya agano, na hasa kushindwa
kuelewa haswa Agano Jipya linahusu nini!
Kwa hiyo mmoja wa waandishi wake amesema kuwa, mji na nchi eti vinawakilisha
mchanganyiko wa miili na maendeleo yao kiroho imefungwa kwa dhambi zao. Kulingana
na mwandishi huyu, nchi hizo zimepewa kanisa ili kwamba eti liwawakilishe wao
mbele za Mungu na kisha kuwaongoza kwenye kutubu na suluhisho! Anapozilinganisha
nchi na miji anatumia usemi kama vile “binti bikira wa Ufaransa” au “binti wa
New York”, analinganisha Ufaransa na mji wa New York. Kwa maneno mengine anajaribu
kutumia maneno ambayo Mungu aliyatumia kwa watu wake aliowachagua, (“bikira,
binti wa watu , watu wangu, binti bikira wa Israel”) ambaye kwake amemwanzishia
agano la uhakika na kwa yeye aliye mkiri. Na kwa ajili yake mtumishi wake alifanya
maombezi. Na mwandishi wao anatumia maneno hayo hayo kwa nchi na miji ya ulimwengu
leo! Kana kwamba leo taifa au mji huo ungeweza kutazamwa kama vile ndio watu
wa Mungu walimotendea dhambi kama ilivyo kuwa katika Agano la Kale; na kana
kwamba kanisa linapaswa kuomba kwa ajili ya mji ule au nchi kana kwamba ilikuwa
ni taifa la Mungu au watu wa Mungu! Inataka kuonekana kana kwamba kanisa linawakilisha
manabii ambao huwaombea watu wa Mungu! Je, taifa la Uingereza au Tanzania linawakilisha
watu wa Mungu au kanisa la Mungu? Na, je kanisa la Bwana leo linapaswa kutenda
kama baadhi ya manabii wa Agano la Kale ili kupata upatanisho kwa ajili ya taifa
kwa kuungama na kutubu dhambi zake?! Mambo haya yote ni mchanganyiko kabisa,
na ni upotoshaji na yanalinyang’anya kanisa huduma lake la kweli. Kama tulivyosema
tayari, matunzo na maombi kwa ajili ya jamii tuishimo ni ya muhimu (yanahitajika)
na ni ya kimaandiko. Lakini tunapaswa kufuata maandiko yanavyofundisha kuliko
kufuata upotoshaji huu.
(Upo mstari mmoja katika agano la kale unaoongelea kuhusu bikira binti wa Babeli,
Isaya 47:1, lakini hii inahusu tu mambo ya hukumu na wala sio maombezi! Na kwa
hakika, katika mstari wote huo, Babeli inachukuliwa kama alama ya utawala wa
kidunia au shetani, ambapo kwake hukumu ya Mungu itatujilia. Soma Isaya sura
ya 13 na 14 hasa mistari ya 4-24, hii inaweza kuelezea lugha iliyotumika katika
47:1. Hakika hakuna mahali popote pale katika Biblia ambapo maungamo au toba
vimefanywa kwa ajili ya dhambi za watu wasioamini; Daniel na manabii wengine
waliwaombea watu wa Mungu! Wanalichanganya kanisa na ulimwengu kabisa.)
Ni nini basi, kwa sababu eti mimi ni Mwingereza, kwa hiyo ninawajibika kuungama
na kutubu kwa ajili ya dhambi ya Uingereza, kama Daniel alivyofanya kwa Israel?
Ni nini basi, kutubu kwa ajili ya lile ambalo Waingereza walilowatendea Wajerumani,
Waispania, Wamarekani, Wa-Irish na wengine wengi katika karne hii, halikadhalika
miaka 100, 200, 500 na 800 ijayo? Inaishia wapi hiyo? Hii, kwa ujumla ni jukumu
lisilokuwa; wanatufundisha kwamba tunapaswa kufanya utafiti wa kihistoria kwa
uangalifu sana na uchuguzi juu ya dhambi kubwa zote, na matendo yasiyo ya haki
ambayo nchi “yetu” imeyatenda, kwa sababu, eti tusipofanya hivyo na kuliongoza
taifa katika kuungama na kutubu kwa dhambi hizo, basi hukumu za Mungu itaendelea
kukaa juu ya nchi yetu na itazuia baraka za Mungu au uamsho kutujia kwa kweli.
(Jambo hili ni udanganyifu). Na kama tutauliza na kwenda mbali kiasi gani nyuma
katika historia, walimu hawa wanatuambia tunahitajika kwenda nyuma mpaka pale
ambapo nchi “yetu” au taifa “letu” lilipoumbwa kwa mara ya kwanza na kugundua
maovu yote makubwa liliyokwisha yafanya toka wakati huo hadi sasa. Kama ni hivyo,
eti twende njia nzima nyuma mpaka kwa Adamu na kutubu kwa ajili ya dhambi zote
ambazo mwanadamu ametenda hadi kufikia wakati huu. Hii inaweza kutimiza kosa
lao la hatari na udanganyifu wao wa kufikiri ambao bado kwa namna fulani tungali
(kupitia maombi ya upatanisho) weza kufidia makosa ya wanadamu, ambayo tayari
Yesu alikwisha yabeba msalabani! Na tukiwaachilia mbali watu wa Mungu Israel,
kabla ya Kalvari, ni wapi katika Agano Jipya ambapo Mungu anahitaji taifa zima
litubu? Hili ni kosa au hitilafu nyingine na udanganyifu. Kama vile wanafundisha
kwamba katika siku hizo za Injili ya Neema, Mungu anatuhitaji tuzingatie ukombozi
wa mataifa kama mataifa, wanafikiri Mungu anashughulika na mataifa leo sawa
sawa na jinsi alivyofanya kwa Israel katika Agano la Kale! Wanafundisha kuwa
eti kanisa linayo haki kutumia damu ya Yesu Kristo kwa dhambi za mataifa, na
wangependa kututaka sisi tuombe kwamba Uingereza kama nchi iweze kupatanishwa
na Mungu kupitia damu yake. Tumekwisha kuona tayari kuwa hakuna kitu chochote
kama hicho ambacho kimefundishwa katika Agano Jipya. Hii si kitu kingine isipokuwa
ni matumizi ya kiushirikina ya damu ya Yesu Kristo.
Hii kwa kweli inaleta upuuzi wa Agano Jipya na ya Injili ambayo ni uweza wa
Mungu uokoao roho wa kila roho na kila mmoja amgeukie Bwana kutoka katika nguvu
za giza na kuibatiza roho hiyo iweze kuingia katika ufalme wa kiroho wa Mungu
wa uzima, furaha amani na haki. Hicho ndicho kinachoelezwa na Agano Jipya -
kuzileta roho katika uzima wa Mungu. Lakini nchi au mji hauwezi ukabatizwa katika
ufalme na uzima wa Mungu. Ndiyo, Injili inaweza kuhubiriwa kwa mataifa yote,
lakini mafundisho na mafunuo ya Agano Jipya ni kwamba mtu ataokolewa kutoka
katika kila kabila na taifa. Haifundishi wala haionyeshi kuwa mataifa hayo yataokolewa
kama taifa pekee katika siku hizi za Injili kama kwamba Mungu analo agano na
Uingereza au nchi nyingine yoyote ile iwayo kama alivyofanya kwa Israel katika
Agano la Kale.
Kanisa siyo ulimwengu; Uingereza siyo Kanisa; na wale wasioamini sio watu wa
Mungu - Danieli aliomba na kuungama kwa ajili ya dhambi za watu wa Mungu, na
wala si kwa ajili ya dhambi za watu wasioamini. Lakini wao wanachanganya yote
pamoja.
Paulo hakwenda Mekedonia na kuliambia taifa la Mekedonia kutubu kwa ajili ya
dhambi zake na vita vilivyopita. Hakuwaita maafisa wa Serikali ili watubu kwa
ajili ya dhambi za nchi yao au mji wao ili kwamba kusababisha upatanisho kwa
mji huo au nchi hiyo. Alitembelea sehemu fulani fulani katika Mekedonia na aliwaambia
watu waishio humo kuwa wanahitajika kutubu dhambi zao na kumgeukia Yesu Kristo
ambaye ndiye atakayewafanya wawe wenyeji wa nchi nyingine, yaani, mbinguni!
Wataweza kuongezwa katika kanisa la Mungu ambao ndio mwili mmoja. Paulo hakuthubutu
kuweza kujaribu kuwafanya Wakristo wa Mekedonia waweze kusababisha aina fulani
ya upatanisho kwa ajili ya nchi yao.
Pasipo kuelewa wanachokifanya au nini hasa wanakisema, wanabadilisha huu wokovu
wa ajabu ambao unawaingiza wake kwa waume wengi katika uzima na uweza wa ufalme
wa Mungu wa mbinguni, kwa mawazo yao ya uanzishaji wa aina ya mambo fulani fulani
ya kiinje tu ya kitaifa au ufalme wa kikirsto.
Baadhi ya waandishi wao wanasema, inapotokea mkristo anatubu dhambi za taifa
lake aishilo, eti hiyo ni hatua ya mwanzo tu; kwa ujumla wasemacho hapo ni kwamba
unapaswa kuwa na maombezi kama Daniel ambaye anazitambua dhambi hizi na kisha
anamuomba kwa ajili ya taifa, hii pia inapaswa kufuatwa na ujumla wa kanisa
ambalo pia linaombwa kuhusu dhambi hizi za taifa. (Wanadai kuwa hii ililetwa
na Ezra ambaye aliwaongoza watu katika maungano ya pamoja); na jambo la tatu
na ambalo, ndiyo hatua ya mwisho ni pale ambapo jamii au maafisa wa kiulimwengu
katika mji ule au taifa wanaziungama dhambi hizo hizo, na hii pia huwakilisha
toba ya kweli ya kitaifa na pia kwamba, kwa taifa hilo! (Na hii nayo wanasema
eti imeletwa na Nehemia katika Agano la Kale ambaye anauwakilisha ulimwengu
au uongozi wa kiserikali!).Wanafundisha hayo ijapokuwa hakuna chochote kile
kama hicho ndani ya Agano Jipya, na kwa ujumla wanalitumia vibaya Agano la Kale
katika kusudi lao la kuunga mkono ubunifu wao. Wakiwa na nia ya kuunga mkono
mambo yao mageni, inaonyesha dhahiri kuwa upotoshaji wao hauna mwisho.
Ni janga la jinsi gani kuona viongozi wa wakristo wengi wakjidanganya wao wenyewe
na tena wakidanganya maelfu ya wengine kwa kufikiri na kufundisha kwamba eti
wanasababisha aina fulani ya upatanisho na kufungua baraka za Mungu kwa taifa
lao pale wanapoungana na kutubu dhambi za taifa lao zilizopita na zilizopo!
Waumini wa Kiingereza waende Australia na kuziungama dhambi zilizopita za waingereza
walizowafanyia waumini wa Australia; kadhalika wakirsto wa Australia waje hadi
Uingereza na kuungama dhambi za Australia walizowafanyia waingereza! Wabrazil
waje Uingereza, Waamerika nao waende Japan, na Wajapan waombe msamaha toka kwa
wakristo wa Marekani na hivyo kuendelea zaidi na zaidi! Wakristo wakizunguka
ulimwengu mzima wakiungama kwa wakristo wengine dhambi zilizopita za “taifa”
lao, ambazo kwa hakika kanisa la Yesu Kristo halina chochote cha kufanya kwake!
“Enyi Wagalatia msio na akili, ni
nani aliyewaloga, ninyi ambao Yesu Kristo aliwekwa wazi mbele ya macho yenu
ya kuwa amesulibiwa?”
Kama tulivyokwisha kuona, hakuna popote katika agano jipya ambapo mkristo anaenda
akizunguka kule na kule kuungama na kutubu kwa ajili ya dhambi za kitaifa za
aina yoyote ile. Hatuuoni mfano wa jinsi hiyo hata mmoja, na wala hayapo maagizo
ya kufanya hivyo yalivyoagizwa na Yesu au hata mitume.
Wakristo toka Roma hawapaswi kwenda Mekedonia kuziungama dhambi za Warumi, wala
kwa Waathemi, kwa Wayahudi au kwa yeyote yule mwingine. Waumini toka Mekedonia,
Athene, bara la Asia au sehemu nyingine hawaendi wakizunguka kuziungama dhambi
zilizopita za watu wao na kuombana msamaha kati yao au nchi nyingine hata kama
walikuwa na historia ndefu ya mapigano kati yao. Ujumbe wa wakristo wa kirumi
hawakwenda Yudea kuomba msamaha toka kwa wakristo wa kiyahudi kule! Ni hakika
kuwa kulikuwepo na mambo mabaya katika eneo lile, kama vile ilivyo katika karne
hii, lakini ukitazama jinsi ambavyo Yesu Kristo amefanya pale Kalvari, basi
kwa kweli ingekuwa ni ukichaa wao kufanya hivyo, ndio maana haishangazi kuona
kuwa hatusemi chohcote cha jinsi hiyo ndani ya Agano Jipya. Na kama ulitaka
kufanya hivyo, utawezaje basi pasipo shaka yo yote kuwa na uhakika kuwa umeungama
dhambi zote ambazo nchi yako imezitenda dhidi ya nchi nyingine? Hata mtaalam
wa historia tu asingeweza kuyaelewa mambo yote ambayo yangeweza kuwa yamemchukiza
Mungu.
Kama watu wa Bwana, sisi sote tu wenyeji wa mbinguni, na tunafahamu kuwa vita
na matendo yasiyo ya haki ya nchi tuishimo hayana chochote cha kulifanyia kanisa
la Yesu Kristo, lakini bado utaona wakristo wengi wakizunguka wakiomba msamaha
wa wakristo wengine kwa ajili ya dhambi za ulimwengu, kwa mfano, dhambi za mataifa
“yao”; wakristo hao je wanaumizwa mioyoni mwao kwa yale ambayo nchi nyingine
zimelifanyia taifa lao? Kwa nini basi waumizwe? Tungepaswa kuwasamehe kama vile
sisi tulivyowasamehe iwapo tunaona kuna ugumu wowote mioyoni mwetu. Mimi sihitaji
mkristo wa nchi yoyote kuomba msamaha wangu kwa ajili ya makosa yaliyofanywa
na nchi aliyotokea kuishi, wala mimi au hata kanisa langu hatuwakilishi Uingereza
kana kwamba tunao uhusiano wa kiagano maalumu na Mungu. Ninajua kuwa wao wanafikiri
kwa kufanya hivyo watakuwa wanasaidia kuleta aina fulani ya mapatano, lakini
hiyo inaishia tu kwenye maungamo mabaya kiroho na kimaandiko ya Neno la Mungu
- bila kutofautisha kati ya ulimwengu na kanisa. Hii ni tafsiri ya mwili ambayo
inakataa kuudhalilisha ukweli kuwa mimi ni uzao wa kutoka juu, tumezaliwa na
Mungu na kwamba wenyeji wetu sasa uko mbinguni (Philipi 3:20). Nimekombolewa
kutoka dhambini na mimi sio wa ulimwengu huu tena, kwa ufahamu wa ndani na ukweli;
mimi sio Mwingereza na wala wewe sio Mtanzania, au Mhehe wala Mmasai; sisi ni
mali ya Mungu (watu wa Mungu). Sitajaribu kujilinganisha na ulimwengu kama vile
mimi ni wake. Hii sio kujifananisha na mahitaji ya wengine, hii ni kuchanganyikiwa,
hii ni udanganyifu mtupu. (Hata kama maelekezo ya dini yanaweza kubeba jina
la ukristo, bado kama watabeba uovu na ukatili watajionyesha kuwa hawana lolote
lile mbele ya kanisa la kristo. Na katika mtiririko wa kuhubiri Injili kwa watu
fulani fulani katika maeneo fulani ya ulimwengu, ukweli huu utahitajika kutolewa
wazi, lakini hii haihalalishi ujumla wa mambo yasiyo ya kibiblia na ya tabia
za ushirikina wa makosa haya ya kisasa.) Kama tulivyokwisha ona, hatuoni mfano
wa aina hii hata mmoja ndani ya biblia yote! Hii haimaanishi kuwa sisi hatujali
au hatuhusiki; la hata kidogo; haimanishi vilevile kwamba hatuwezi kuomba kwa
ajili ya hayo, kwa ajili ya jamii zetu au nchi. Na tutaweza kuona baadaye jinsi
kanisa linavyopaswa kuomba kwa njia za aina gani ili kwamba wale ambao hawajaamini
wapate kufikiwa na Injili! Lakini ulimwengu, na zaidi sana kanisa halisaidiwi
kwa mawazo hayo potofu ya kibinadamu, ambayo yanatumikia tu mambo magumu yasiyofahamika
na kuharibu ukweli na uweza wa Injili.
Lakini waumini hao wanaendesha mikutano hii ya maungamo na kutubu, wao wanasema
kuwa, eti wametembelewa kwa macho na wanaamini kuwa eti ni Mungu anayetembea
katikati yao na kuguswa mioyo yao. Lakini wakiwa wakidanganyika kwa kuamini
kwao wenyewe. Ndio maana haishangazi kuona kuwa wanapokusanyika pamoja wanazidi
kujidanganya kwa mambo yanayodhihirishwa na kujisikia. Na kwa hakika hii ni
jambo la hatari na sisemi mambo haya kiurahisi rahisi tu. Lakini aina hii ya
makosa na udanganyifu yanapatikana nyakati hizi za Agano Jipya ambapo waumini
kwa kutaka kukidhi nia zao na mawazo yao, kwa kweli kwa kufanya hivyo wanakuwa
wanajifungulia wenyewe mlango ili kupokea Injili ya tofauti, Yesu wa tofauti,
na Roho wa tofauti - na wao wanafikiri kuwa hayo ni ya Bwana! Lakini mtume Paulo
anaonyesha hatari ya jambo hili kwa kusema kuwa kwa kweli wanadanganywa na malaika
wa nuru, ambaye mtume Paulo anamlinganisha na shetani (2 Kor.11:1-15). Na hivyo
ndivyo ilivyo leo kwa waumini hawa. Ni waumini, lakini wanauacha ukweli na wepesi
wa Injili ya Yesu ambayo walikwishaipokea hapo mwanzoni. Wanajiweka wazi wao
wenyewe kwenye udanganyifu. Haishangazi kuona kuwa wanaweza wakawa na aina zote
za ujuzi ambao utawaendeleza kudanganywa tu. Bali kujisikia huko wanakojisikia
pamoja na kudhihirishwa kwake kunatokana na pandikizo la Injili nyingine na
roho mwingine.
Kaka zangu na dada zangu katika Kristo ninawasihini kwa ajili ya faida ya nafsi
zenu ambayo kwayo Yesu Kristo alikufa Kalvari ili kukomboa na kuwaweka huru
na kutufanya tuwe wake mwenyewe: mjihadhari na mafundisho hayo na madanganyo
yake.
Biblia na kile inachosema ni cha muhimu zaidi kuliko shirika lolote kubwa la
kikristo au wanenaji. Haijalishi jinsi gani wanenaji hao wanafahamika au kujulikana.
Na kama basi ni bora uchukue mwelekeo wa Kristo, kuliko kufuata kile ambacho
kinajulikana lakini na hakifundishwi katika maandiko ya neno la Mungu, na kile
unachofikiri kuwa kitatueletea umaarufu na kufahamika zaidi.
“Ushahidi” wa Maandiko Yao
Maandiko ya neno la Mungu kwa uhasa ni kitu gani basi? Je, hawa walimu wanatupatia
sisi ili kuonyesha kuwa kanisa linapaswa kuungama na kutubu kwa ajili ya dhambi
(zilizopo na zilizopita) za nchi tuishiyo? Tumekwisha kuona nukuu fulani kutoka
Daniel. Wengine wananukuu mistari inayoonyesha fadhili za Mungu katika kuwabariki
wamataifa kwa wokovu, kama vile, Mwanzo 12:3, Zab. 22:27, Isaya 56:7, Yona 4:11
na Warumi 15: 9. Kwa hakika tungeweza hata kuongezea mistari hiyo na mingineyo
inavyoonyesha, kama vile, kwamba tokea mwanzo Mungu alipanga kuwabariki watu
wote katika dunia, lakini hakuna hata mstari mmoja kati ya hiyo, inayoonyesha
kwa namna yoyote ile kwamba watu wa Mungu wanapaswa kuungama na kutubu kwa ajili
ya dhambi za mataifa hayo, kabla Mungu hajawabariki kana kwamba hiyo ndiyo inayomfungulia
Mungu mlango wa kuja kuwabariki! Ingawaje Mungu ameahidi kupanua wokovu wake
kwa watu wote, lakini jambo hili haliwakilishwi ndani ya maandiko ya neno la
Mungu kwa njia ya vifungu vipya vya kisheria kama ile ya pale Sinai na ambayo
mataifa yasiyoamini yanapaswa kuitunza - na kanisa kuombea kwa ajili yao iwapo
hawayatunzi! Hapana! Makubaliano ya Agano Jipya ambayo Mungu anayapanua kwa
mataifa yote sasa, ni kwa ajili ya yeyote yule aaminiye, waume kwa wake wanaokolewa
kwa imani katika Kristo Yesu, huru kwa neema ya Mungu. Huu ndio msingi wa Agano
Jipya; toleo la Yesu Kristo ni kwa ajili ya waume na wanawake na ya kwamba,
yeye ndiye aliyesulubiwa na akafufuka ni mlango wa agano hili, wala hayapo kabisa
masharti ya kutimizwa kabla na kubarikiwa kwa wokovu wake.
Hayupo mpatanishi wa agano awaye yoyote yule na wala halipo agano lingine! (Mstari
niliyoielezea hapo juu, haiwakilishi aina fulani ya uhusiano wa agano ambapo
Mungu anasema, “kwa sababu nimekuahidi kukubariki wewe kwa wokovu kupitia Kristo
tangu milele (Tito 1:2) basi, sasa umo katika uhusiano wa kiagano na mimi na
kutokana na agano hilo kwa kweli huwezi kupokea wokovu kamili mpaka kwanza nchi
unayoishi itakapotubu dhambi zake, zilizopita na zilizopo).
Kwa hakika yapo Agano la Kale na Agano Jipya tu. Hakuna lingine! Je, wewe umo
ndani ya agano lipi kati ya hayo mawili? Aina hii ya kuomba kwa ajili ya dhambi
za taifa zilizopita ni makosa, baadaye tutaangalia kwa karibu zaidi, jinsi Mungu
anavyotimiza kusudi lake ili kubariki wale wasioamini.
Wanaonyesha vidole kwa Yona, alipokuwa akihubiri kwa watu wa Ninawi, lakini
hapo anathibitisha tu yale tunayoyasema katika makala hii, yaani, ni kwa kulileta
neno la Mungu kwa watu wenyewe, ndiyo inayowapatia fursa kwa imani na toba.
Yona aliongea moja kwa moja na mioyo yao na akawaambia watubu. Nao watu wote
pamoja, yaani, mji mzima, walitubu kwa ajili ya dhambi zao. Walitambua na wakakiri
dhambi zao mbele ya Mungu. Yona hakuwaambia kwamba, kwanza watubu katika ujumla
wao kwa ajili ya dhambi za wengine (wenzao waliomo mjini) kabla hajawabariki
na kuwasamehe.
Wananukuu Kut.10:16-18, wakisema eti mbona Musa aliwaombea kwa Farao, na kwa
hiyo kanisa nalo linapaswa kujitambulisha na dhambi za taifa na kutubu kwa niaba
yao! Ndiyo, ni kweli kwamba, Musa aliomba kwa ajili ya Farao kwa sababu alizikiri
dhambi zake na akamsihi Musa aombe kwa ajili yake. Hiyo inatofautiana sana.
Musa alikuwa hatubu kwa ajili ya dhambi za mtu asiyeamini, na cha muhimu zaidi
kwa wakati huo, Yesu alikuwa hajafunuliwa kuwa ndiye mwombezi kati ya wanadamu
na Mungu. Hivyo ilikuwa ni jambo la kawaida kuona kuwa Farao amsihi Musa ili
aombe kwa ajili yake, hasa pale ambapo Musa alipokuwa akifanya na kuongea kwa
niaba ya Mungu kwa ajili ya watu (Ku. 4:16). Kwa hiyo huu hauwezi kuwa ni mfano
wa mafundisho yao hayo, agano lisilosahihi, iwapo wataendelea kana kwamba Yesu
hajafunuliwa kutoka mbinguni kuwa kama mwokozi na mpatanishi wa wanadamu. Hapa
pia tunaona jinsi mafundisho hayo yanavyojaribu kumweka mpatanishi mwingine
zaidi ya Yesu Kristo kati ya Mungu na wanadamu kwa ajili ya toleo la dhambi.
Wanafanya hivyo hivyo, pale wanapotaja kuwa Musa alipokea msamaha kwa ajili
ya dhambi za Waisrael katika (Hes.14:17-21), na wanazidi kutuambia kwamba eti
kanisa linaweza kupokea msamaha wake kupitia maungamo ya dhambi za kitaifa,
kwa ajili ya dhambi za mataifa hayo, kama vile Musa alivyofanya kwa Israel!
Hapa wanajifanyia kosa la kidole, wanachanganya tena ulimwengu na kanisa, wala
hawawezi kutambua kama iwapasavyo kutambua kuwa leo yupo mpatanishi mmoja tu
kati ya Mungu na mtu, na huyo ni KRISTO YESU. Tunaelewa kuwa huduma ya Musa
ilikuwa ni picha ya kielelezo cha awali cha Kristo na kwa maana hiyo alikuwa
ni wa namna ya pekee kabisa kama tunavyoona katika Kut. 4:16; Hes.12:6-8 na
Kumb. 18:15.
Katika Agano Jipya, wanamnukuu Yesu, akimwomba Baba awasamehe wale waliomsulibisha
(Luka.23:34), lakini pale Yesu alikuwa hafanyi lolote zaidi ya lile alilofundisha
yeye mwenyewe kufanya.; kama vile, kuwasamehe wale wanaotutendea mabaya kwa
makusudi, hasa pale wanapokuwa hawana wazo kuwa wanatufanyia ubaya. Ninafahamu
kuwa, sisi kama wakristo, sote tumemfuata Kristo katika hili; lakini hata hivyo
hii haiwakilishi ushahidi wa Agano Jipya kwamba kanisa sasa linapaswa kujishughulisha
na kutubu kwa ajili ya dhambi za miji au nchi yao! Zaidi ya kushangaza, ni pale
tunapoona wanamnukuu pia 1Yoh.1:9, “…tukiziungama dhambi zetu…”, na wanasema
bila woga au hofu ya Mungu kuwa eti mstari huo unatuonyesha kwamba, kanisa la
kwanza lilikuwa linajishughulisha na Ibada za maungamo ya dhambi za jamii! Wanadai
kuwa, wakristo hapo walikuwa wanabeba mila /desturi za Agano la Kale zilikuwa
ni mfano wa pekee kwao walioufahamu na kuusikia! Zile “mila” ambazo wanazizungumzia,
ni mfano wa pekee wa mtu kama Danieli au Nehemia akiomba wakati ule wa kutawanywa
na kupelekwa uhamishoni kwa Israeli. Lakini hii ilihusiana tu na Israeli na
kwa wakati ule wa pekee katika historia yao! Nini? Baada ya Kalvari na baada
ya kumpokea Roho Mtakatifu Wakristo walikuwa bado hawajapata ufahamu wa ndani
zaidi kuliko tukio hili la pekee la Agano la Kale? Hii inaweza kuwa ni kweli
kabisa kuhusiana na walimu hawa wa siku hizi lakini sio mitume wa kanisa la
kwanza. Hii ni aina ya rushwa ya Neno la Mungu na kwamba sisi hatulazimiki kuukubali.
Lakini labda inatosha kusema kuwa, Yohana anatumia uwingi, kama vile asemapo
“sisi ” na “zetu” katika barua zake zote akimaanisha kuwa, watu wa Mungu - au
je, tunapaswa kusema kwamba jamii ya watu wasioamini wale wanaotuzunguka, wanao
ushirika pamoja na Baba na Mwana? (1Yoh 1:3)!!?
Na hii ndiyo baadhi ya mistari yao muhimu sana ambayo kila mara hutolea mifano
yao, au kuthibitisha mafundisho yao. Lakini pia hii inatuonyesha sisi wazi tu
kwamba, hata hao walimu hawawezi kutoa mfano, kwa kweli hapana hawana hata mfano
mmoja ambao watu wa Mungu wameonekana sehemu fulani wakiungama au kutubu kwa
ajili ya dhambi za nchi nyingine au kwa ajili ya dhambi za wasioamini wowote
wale. Sasa kumbe tunaona kwa uwazi zaidi hapa kwamba kwa hakika wanakuwa hawapendezwi
na kuelekezwa kutoka katika maandiko ya neno la Mungu katika mambo haya; bali
wao wanatumia andiko lolote lile wanalofikiri kuwa litaweza kutimiza kusudi
lao, na iwapo halitimizi kusudi lao, basi wao hulilazimisha ili liweze kutimiza,
kwa kuyumbisha maana halisi ya Neno lile ili kwamba lipate kulingana na mtindo
wa mafundisho yao.
Baadhi ya Waraka wa Msingi
Sasa, hebu tuyaangalie mambo ambayo wao huyachukulia kama msingi wa mfumo wao
wote wa kufikiri na kufundisha kuhusiana na habari hii ya maungamo ya dhambi
ya kizazi kilichopita. Mstari wanaoupenda sana kuutumia kama msingi wa mafundisho
yao, unapatikana katika Mambo ya Walawi 26:40.
“Nao wataukiri uovu wao na uovu wa baba zao…” (Hapa unatakiwa usome sura nzima
wewe mwenyewe).
Ukitazama kwa makini. Katika sura hiyo, Mungu anatamka hukumu atakayoileta kwa
Israel, iwapo tu kama watakuwa wakirudiarudia kutomtii. Na hukumu ya mwisho
itakuwa ni kuwa Mungu atawafunua wazi kutoka katika nchi yao na kuwatawanyia
katika nchi nyingine mbalimbali; lakini hata hivyo, atakuwa bado na huruma juu
yao na kukumbuka agano lake iwapo watatubu na kuziungama dhambi zao (mstari
wa 40-41).
Kwa mapana zaidi ndani ya mstari huu walimu hawa wa kisasa wanajaribu kusimamia
na kutengeneza mawazo ya “upatanisho wa maungamo na toba” na maungamo na toba
ya dhambi za kihistoria, kwa pamoja, wao wanafundisha kuwa, Mungu kwa hakika
eti hawezi kumbariki mtu au taifa mpka kwanza taratibu hizo ziwe zimekamilishwa.
Kama vile kanisa linaongoza njia kuelekea kwenye kuungama na kutubu kwa ajili
ya dhambi za taifa na wanaamini kuwa hii itaweza kusafisha njia kwa maungamo
ya kiulimwengu kwa ajili ya hizo dhambi za kitaifa. Lakini hayo yote pengine
hapa hatuna nafasi ya kuzitazama sababu zake kwa nini iwe hivyo.
Wanawanukuu baadhi ya watu kama mifano ya aina ya maungamo na toba; haishangazi
kuona wanawataja akina Daniel, Ezra, Nehemia na Yeremiah (kama vile katika Daniel
9:;16) ambapo wote wanazikiri dhambi za mababa zao ndani ya maombi yao. Mstari
tulioutaja hapo juu unapatikana pia katika kitabu cha Mambo ya Walawi pamoja
na mifano ya maombi ya watu hao, yanawakilisha jiwe la msingi la mafundisho
hayo hayo. Lakini kwa nini tunasema, haishangazi kuona kuwa wanawanukuu watu
hawa maalumu. Ni wazi kuwa iwapo tutaisoma sura hiyo - Walawi 26 - na mistari
hiyo katika mtiririko wa habari zao, ni wazi kutoka kwa Mungu mwenyewe kwamba
aina hii ya maungamo (ya dhambi za pamoja na vizazi vilivyopita) ingeweza kutokea
katika muda maalum ndani ya historia ya Israel, yaani, wakati Mungu alipowanyanganya
na kuwatapanyatapanya mbali katika nchi nyingine, (Walawi 26: 27-42). Hivyo
ndivyo tunavyogundua kwa uhakika pale, tunaposoma sura hiyo na kuiacha Biblia
ijitegemee (isema nasi) badala ya kuitumia ili kuunga mkono mawazo yetu wenyewe
tu. Kwa hiyo haishangazi kuona kuwa hawamnukuu mtu mwingine awaye yote, anayeomba
kwa jinsi hiyo kabla ya wakati wa Jeremiah, (ambaye yeye katika wakati wake,
Mungu alikwisha anza kutimiliza hukumu yake dhidi ya Israel, kwa kuwatapanyatapanya),
kwa sababu hakuwepo yeyote alifanya hivyo, kwa kuwa Mungu hakutazamia hayo kabla
ya utawanyo!
Katika mazingira ya namna hii, kukataliwa na kupelekwa uhamishoni, ambavyo vinawakilisha
kuvunjika kwa agano, kungekuwa ni nini tena cha kawaida zaidi ya hii, yaani,
Mungu angewataka wao kutambua na kukiri kama vile kuungama kwa sio tu dhambi
za kizazi kimoja bali kule kurudiarudia na kutokuwa na utii kwa vizazi vingi
vilivyoanzia kwa Israel wakifukuzwa kutoka katika nchi yao. Mungu aliwataka
waelewe kuwa hii haikuwa tu adhabu kali na ya ghafla kwa sababu ya kizazi kimoja;
bali kwamba vizazi vingi vinageuza migongo yao kutoka katika toleo la neema
yake ya uvumilivu wao wa muda mrefu.
Iwapo tutasoma Walawi 26 tutaweza kuona namna gani Mungu alivyokuwa mvumilivu
na mwenye rehema kwa Israel. Anawaambia kuwa ikiwa atakataa kumtii na kumfuata,
ndipo atatuma aina fulani ya hukumu juu yao. Kwa nini? Ni kama adhabu tu na
laana inayoendelea? Hapana! Tunapoangalia ugumu wa mioyo yao, Mungu angeweza
kutuma hukumu kuwafanya wao wafikirie upumbavu wa njia zao na hivyo iweze kuwapa
fursa ya kutubia dhambi na uovu wao; ili yamkini, waweze kumvumilia yeye. Na
kama watakataa kuchukua tahadhari ndipo atazidisha ugumu au ukali wa hukumu
hizo, katika kujaribu kuwafanya watambue kuwa walikuwa mbali toka Mungu na baraka
zake za ajabu. Hivyo, kutokana na hukumu hizi Mungu alitaka kuona kuwa Waisrael
wanarejea katika ufahamu wao kisha kurudi kwake, kama vile yule mtoto katika
Luka 15. Tazama walawi 26:14,18,21,23,27. Katika hayo yote, tunaona kuwa hukumu
zote hizo kwa kweli zilikuwa ni njia ya Mungu ya kuelezea Rehema zake, katika
maana ya kuwa alitaka kutengeneza fursa ya aina fulani kwao ili waweze kujitambua
upumbavu wao (upuuzi wao) ili watambue na watubu na kisha wamrudie yeye.
Kwa hiyo tunagundua hapa kuwa , kabla ya wakati wa Uhamishoni, ikiwa ikitokea
mfalme yeyote wa Israel au Yuda pamoja na watu kama vile kizazi kizima chochote,
wakatubu na kurejea kwa Mungu ndipo Mungu aliwabariki na ndipo waliweza kubarikiwa,
pasipo maungamo au kutaka kuungama dhambi za vizazi vilivyopita. (Ijapokuwa
ingewezekana kuonekana kama ni jambo la kawaida kuzitaja dhambi za aina hii
kama wangekuwa wamefuta hizo dhambi zao binafsi; sio tu ili kuomba waweze kupata
msamaha zaidi au kuachiliwa, bali tu kama utambulisho wa yale yaliyowahuzunisha
kwa hakika, na pengine yalihitajika kusafishwa kutoka nchi iliyoanza mapema.)
Hata hivyo, hatuoni mfano wowote wa aina hii ya maombi kabla ya mtawanyiko,
kwa mfano, nyakati za mfalme Asa, Uzia, Hezekia na Josia. Tunawaona hapo wakimrudia
Bwana pasipo hata kuzikiri dhambi za mababa, na hiyo ndiyo tunayo iona ndani
ya Biblia yote. Hii ndiyo kipimo chenyewe kuwa mtu azitubie dhambi zake mwenyewe,
sio za mtu mwingine. Na ingawaje Yeremiah anaonekana kuziungama dhambi za mababa
ndani ya muda huo wa mahangaiko ya Israel, mzigo wake mkubwa na maelezo ya ujumbe
wa Mungu kwa watu wake Mungu kwa wakati huo ni kwa ajili ya mioyo yao wenyewe,
ikiwafunga, ikiwahimiza na kuwainua ili watubu na kumrudia Bwana.
Tukirudia kwenye maelezo ya mwanzoni tunaona kuwa Mungu hakuwatawanya Waisraeli
kwa sababu ya dhambi za kizazi kimoja, bali alichoshwa na vizazi vingi vilivyo
mgeuzia mgongo Mungu; na mwishoni mwake kulikuwa hakuna chochote ambacho Mungu
angeweza kufanya, bali ni kuwaondoa katika nchi kama alivyokwisha kusema. Mungu
alimwita Israel, “mtoto wake” ambaye amemkomboa kutoka Misri (Hosea 11:1). Naye
alifanya agano pamoja nao pale Sinai, walikuwa ni taifa moja na ni watu wake,
naye alijishughulisha nao kama wana wake au kama bibi arusi wake, na alikuwa
amewaahidi na akawapa nchi ya Kanaani kama sehemu ya agano lake pamoja nao.
Lakini baada ya kuvumilia dhambi na ibada yao ya sanamu kwa muda mrefu, ilimbidi
Mungu awatoe katika nchi yao. Na kwa kweli jambo hilo lilikuwa na maana kubwa
kwa sababu wao kumiliki nchi ile ilikuwa ni sehemu ya agano ambalo Mungu alikuwa
amelifanya na Israeli na sasa hili agano likawa limevunjwa na Waisraeli kukosa
uaminifu. Na sasa baada ya kuwa wametawanywa nchi nyingine, walipaswa kutambua
kuwa kuendelea kwao kukosa uaminifu kwa vizazi vingi kulikuwa kumepelekea wao
kutolewa kutoka katika nchi ya ahadi. Watu kama Daniel, Ezra na Nehemia (Ezra
9:1-10, hasa mstari 7, pamoja na Hezekiah katika 2 Mambo ya Nyakati 30:6-9)
walitambua mambo hayo, yaani, ilikuwa ni uasi wa mara nyingi wa Waisrael (wakati
wa vizazi vingi) ndio uliowapelekea kwenda uhamishoni. Na kufuatana na Walawi
26, wakaungama kule kutokuwa na utiifu kwao kwa vizazi vingi. Aina hii ya maungamo
ilionekana pia katika Kumb. 30:1-5, 1 Falme: 8:46-50, ingawaje katika sura hizo
hatuoni popote wanapotaja maungamo ya dhambi za mababa.
Kwa hiyo, hapa katika Agano la Kale, walichokifanya akina Daniel na wengineo
ni kuungama au kukiri dhambi zilizopita za kisraeli zilizosababisha uhamisho
na kutokumilikishwa, ambazo kwa sababu wanazigundua wao wenyewe. Hata nyakati
za Nehemia, Israel na Yuda walikuwa ni watu waliotapanywa na ile nchi ya ahadi
ilikuwa inakaliwa. Kama nilivyokwisha sema, hapo juu, kile tunachokiona katika
nyakati za misukosuko ni kuziungamia sababu ya misukosuko hiyo. Kwa hiyo tunaona
kuwa kukiri uasi uliofanywa na Waisraeli kwa vizazi vingi kulihusishwa haswa
na wakati ule Waisraeli walipotawanywa na kupelekwa uhamishoni, muda ambao waisrael
walikuwa hawamiliki nchi. Hata hivyo, wengine wao waliruhusiwa kurudi. Hii ilifanana
na wakati ambapo agano lilivunjwa - agano maalum lililofanywa kati ya Mungu
na Israel, sio kati ya Mungu na mataifa nyingine!
Hebu sasa tulielewe vizuri jambo hili. Kwenye Biblia ndani ya Agano la Kale
na Jipya hakuna po pote pale ambapo watu wa Mungu wanaungama au kutubu kwa niaba
ya dhambi za watu wasioamini – za zamani au za sasa, huko vijijini kwao, mjini
au katika Taifa – ili waweze kupata aina fulani ya Upatanisho kwa ajili ya nchi.
(Tumekwishashughulika na Musa akiomba kwa ajili ya Farao). Hakuna mfano wo wote,
hakuna maagizo yo yote ya kufanya hivyo. Hakuna mahali po pote pale ambapo watu
wa Mungu wanatubu kwa ajili ya dhambi za kizazi kilichopita, iwe kwa ajili ya
waaminio au wasioamini. Hili ni jambo lisilowezekana. Ni katika mazingira ya
aini moja tu ambapo Mungu anawategemea kuungama dhambi za vizazi vilivyopita
vya watu wa Mungu – na huu ulikuwa ni wakati wa Uhamishoni na Utawanyiko. Hakuna
wakati mwingine wo wote ule wala katika aina yo yote ile ya mazingira ambapo
tunasoma kuwa watu wa Mungu walipodiriki hata kuungama tu dhambi za vizazi vilivyopita;
ili kupata aina fulani ya Upatanisho au baraka. Ukweli huu pekee ni zaidi ya
kutosha, kuonyesha jinsi mafundisho haya ya kisasa yaliyokosewa na jinsi yalivyosimamia
katika hila.
Fundisho la Ezekiel: Sura ya 18
Kwa nini Israel walichukuliwa uhamishoni? Je ni kwa sababu tu ya dhambi za vizazi vilivyopita? Je walikuwa wakiadhibiwa kwa ajili ya dhambi za mababu zao? Mungu akizungumza kupitia Ezekiel katika sura ya 18 anatuambia waziwazi kwamba walikuwa hawaadhibiwi kwa ajili ya dhambi za mababu zao! Kupitia Ezekiel, Mungu hasa alikuwa akiwakemea watu wake kwa kufikiri na kusema kitu kama hicho! Kila mtu hubeba hukumu kwa dhambi zake tu. Kama Yuda wangekuwa wametubu na kumgeukia Bwana na moyo wao wote wakati wa Yeremia, basi Mungu angekuwa amewabakiza na kuwabariki kama ambavyo alikuwa amefanya kabla - Yeremia 26:1-7, hasa ya aya 3. Lakini ukweli ni huu, kwamba kizazi kile kiliendelea katika miungu na uasi kinyume na neno la Mungu, kama vile vizazi vingine vilivyokuwa vimefanya. Ulikuwa ni uasi ulioandikwa wa vizazi vingi, ikiwa ni pamoja na hiki, kilichosababisha uhamisho.
Lakini hata kwa Israel mwenye kurudi nyuma, Mungu katika wema wake atangaza rehema zake na kuwataka wamgeukie na warudishwe katika nchi yao, Yeremia 3:12-14. Katika mafungu haya ya maneno na katika mengi mengine katika Biblia yote, Mungu anasema na watu juu ya dhambi zao na jinsi gani wazitubie njia zao na kumgeukia. Mungu hataji kamwe toba juu ya dhambi za mababu zao. Hakuwaamuru kukiri dhambi za mababu zao kama kitu ambacho wangetakiwa kukifanya kwa kawaida. Kama tulivyoona katika Lawi 26:40, Mungu aliwategemea kuungama dhambi zilizokuwa zikirudiwa na zilizolundikwa kwa wingi kwa vizazi vingi ambazo zilisababisha wafukuzwe toka nchi ya ahadi. Huo ulikuwa wakati pekee na kwa sababu maalum ambazo tayari tumezitaja.
Ilikuwa ni watu wa Israel wenyewe
waliofikiri vibaya kuwa walikuwa wanabeba uovu wa babu zao - kwamba walikuwa
wanaadhibiwa kwa ajili ya dhambi za baba zao; “Baba wamekula zabibu mbichi,
na watoto wakatiwa ganzi la meno.” - Ezekiel 18:2. Haya ndiyo maneno Israel
walikuwa wanasema, na hata walibishana na Mungu juu ya hayo katika Ezekiel 18!
Mungu hakufurahishwa hata kidogo na mawazo yao hayo maovu. Na kila kitu ambacho
tumekisema hapo juu kinaungwa mkono pia katika sura hii, na kuwekwa hasa katika
muhtasari katika mstari 19-23. Na mstari wa 20 unatangaza:
“…..Mwana hatauchukua uovu wa baba yake, wala baba hatauchukua uovu wa mwanae…..”.
Na katika sura hii tunaona lile ambalo ni kweli katika Biblia yote, yaani kwamba,
kila mtu anawajibika kwa dhambi yake na anaweza tu kutubu dhambi yake. Hakuna
haja ya kutubu kwa ajili ya dhambi ya babu zetu, kwa sababu hatubebi uovu wao
au hata adhabu kwa ajili ya dhambi zao. Katika Biblia hii ndiyo kawaida – kwamba
watu watubu dhambi zao, na si za mwingine! Ingawa Yeremia anaungama dhambi za
mababa wakati wa kutawanywa Israel, mzigo uliolemea na kilichokuwa kwenye ujumbe
kwa watu wa Mungu kwa wakati huo ni kwa mioyo yao wenyewe, akiwataka waache
ugumu wa mioyo, akiwasihi waache dhambi yao, akiwakazia watubu na kumrudia Bwana.
Haya ndiyo yaliyomo katika huduma yake - kuonyesha Israel, wakati huo, dhambi
na kutangazwa kwa rehema na hukumu ya Mungu. Na tunakuta hili ni sawa katika
Biblia yote. Ukisoma Yeremia na manabii wengine; ukisoma Wamuzi, Wafalme na
Mambo ya Nyakati; ukisoma Agano Jipya; utakuta neno la Mungu huja kupitia watumishi
wa Mungu wakiwasihi watu waliotenda dhambi warudi, au warudi kwa Bwana; neno
huja kwa watu wenyewe juu ya dhambi zao wenyewe, likiwashashiwi juu ya dhambi
zao na kuwataka watubu na si kuwataka watubu dhambi za mwingine awaye yote.
Na kwa hiyo tunaona mtu mmoja mmoja na jamii wakitubu dhambi yao na kupokea
baraka za Mungu pasipo kutajwa kwa dhambi za vizazi zilivyopita – wakiwa waaminio
au wasioamini! Hii ndiyo hali ya kawaida. Lakini mafundisho haya mapya yanachukua
kile kisicho cha kawaida (kilichohusu wakati wa utawanyiko), inavuruga kabisa,
na kufanya iwe kanuni - inafanya iwe sheria na kongwa kwa watu wa Mungu! Lakini
tena katika hali zote hapo juu, tuone kuwa ni swala la manabii wakiweka mkazo
na kuwaombea watu wa Mungu – si kwa ulimwengu, si kwa wasioamini. Je hawa waalimu
wetu wa kisasa hupata kutoka wapi mawazo yao hayo? Hasa katika Agano jipya,
kifo cha Kristo pale Kalvari kinashughulikia maisha yetu ya nyuma na kutukomboa
toka wakati uliopita – 2 Kor.5:17,18; Rumi 6:6; 1Pet 1:18 - tunapomgeukia na
kuzaliwa mara ya pili. Msalaba wa Kristo kukatwa kwetu kutukufu toka dhambi,
toka hatia yake, hukumu kututawala katika maisha yetu, na kutoka kuhukumiwa
kote. Ni mahali pa kukatwa toka dhambi za baba zetu – hadi mpaka Adamu - na
hukumu zote zinazoendana nazo. Nguvu ya msalaba ni kuu kuliko tunavyofahamu,
Efeso 1:16-23. Ni nguvu ya Mungu kila aaminiye, na hakika hakuna haja au hitaji
la kutubu kwa ajili ya dhambi za baba zetu, kwa sababu kifo cha Kristo kimeshughulikia
dhambi zote na hatuwezi kujipatia upatanisho zaidi kwa toba ya jinsi hiyo -
si kwa ajili yetu na wala si kwa mji au nchi tunayoishi. Na dhambi ya mababu
zetu na hukumu kwa ajili yake haiwezi kutugusa kama sisi ni wa Kristo. Tuko
huru kwa sababu Mwana ametuweka huru. Mafundisho haya mapya yanataka tu kuturudisha
nyuma kwenye kongwa.
Katika Yeremia 31:29-34, Mungu anasema kitu kilekile ambacho alisema kupitia
Ezekiel 18. Mungu anawaambia kwamba siku inakuja ambapo hawatatumia mithali
hiyo tena, ambayo ni, watoto wakatiwa ganzi la meno kwa sababu baba walikula
zabibu mbichi. Mungu alitaka wasiendelee kulaumu vizazi vilivyopita kwa ajili
ya dhambi zao! Sasa Mungu anawaambia juu ya Agano Jipya ambalo anakwenda kuweka
ambapo katika hilo atasamehe uovu wao na asikumbuke dhambi yao tena. Hii ni
ajabu na wazi, lakini akizungumza kuhusu mistari hii, mmoja wa wasomi hawa wa
kileo anasema kwamba Kalvari na Agano Jipya haviondoi haja ya kuungama dhambi
za baba zetu na zile za miji na nchi tunazoishi ndani yake! Hata licha ya yaliyosemwa
katika 1 Pet 1:18, anafundisha, sambamba na wengine, kwamba wana na jamii bado
wanaathirika na hukumu ambazo zinahusu dhambi za mababa na vizazi vilivyopita
na kwamba kwa hiyo tunaweza tu kujipatia upatanisho kamili na kupata baraka
kamili za Mungu kupitia kutubu dhambi hizi za wakati uliopita!
Msomaji mpendwa, ni nini kinachoweza kufanywa au kusemwa watu wanapompinga Mungu
na kweli yake moja kwa moja. Mungu anasema kitu kimoja nao wanasema,"Hapana
si hivyo".
Kutoka 20: 3-6
Sasa tumefikia fungu lingine la maneno ambalo waandishi hawa wa kileo wanalihesabu
kuwa lenye umuhimu wa msingi wa mafundisho yao, si kuhusu kutubu dhambi za kitaifa
na za mababu peke yake, lakini pia kuhusu laana na kile wanachokiita “roho za
eneo”. Sehemu wanayoilenga hasa ni pale wanapozungumzia dhambi za mababa zikiwafikia
wana hadi kizazi cha tatu na cha nne. Toka fungu hili, pamoja na Lawi 26:40,
wanaanzisha usemi mpya ambao haupo kwenye Biblia. Wanaita dhambi hii, "dhambi
ya vizazi". Kwa usemi huu hawafanyi rejea kwenye sheria ya dhambi na mauti
ambayo imekuwa ikitenda kazi katika kila mtu tangu anguko la Adamu, na kwa hiyo
Kristo alikufa na kutusafisha na kutuweka huru. Hapana. Kutokana na fungu hili
hufundisha kuwa kama kizazi kimoja au mtu akitenda dhambi au kuabudu miungu,
basi dhambi hiyo na hukumu yake, huendelea katika kizazi kinachofuata, kwa njia
ambayo itazuia baraka za Mungu na kuleta hukumu. Na kwa sababu ya Lawi 26:40,
wanasema kwamba dhambi hizi za vizazi vilivyopita zinatakiwa zitubiwe! Wanasema
mistari hii miwili toka Kutoka na Walawi, inahusu watu wote - Myahudi au Myunani,
mtakatifu au mwenye dhambi - tangu Mungu alipoweka sheria kwa Israel pale Sinai,
mpaka siku ya leo! Wanafundisha pia kwamba Kalvari haijabadilisha hitaji la
kuzitubia dhambi za vizazi vilivyopita. Kama hatufanyi hivyo, basi dhambi za
vizazi vilivyopita na hukumu zake, bado zinatuathiri na bado zinatufanya tukose
baraka kamili za Mungu na pia hutupatia msingi wa kisheria wa Ibilisi kufanya
kazi katika maisha ya watu na jamii zao! Lakini yote hii ni tafsiri isiyozekana
ya mafungu haya.
Tumekwisha kuona tayari kiasi gani jambo hili ni kosa kabisa na utunzi. Tumeona
pia jinsi ambavyo wanatumia vibaya kabisa Lawi 26:40. Sasa, tunapoendelea kutazama
fungu la Kutoka 20, tunakuta hakuna amri kwa watu wa Mungu kutubu kwa ajili
ya dhambi za mababa. Wazo hili wala halijatajwa katika kutoka 20. Mungu anatangaza
kwa Israel kwamba yeye ni Bwana Mungu wao aliyewatoa Misri. Mungu anawaonya
wasiwe na miungu mingine zaidi yake kwa sababu yeye ni Mungu mwenye wivu, ambaye
huwapatiliza wana mabaya ya baba zao hata kizazi cha tatu na cha nne cha wamchukiao.
Nguvu na uzito wa maana ya mstari wa tano (ang. Kumbu. 5:9), iko juu ya hao
wamchukiao. Wale wanaondelea kumkataa Mungu na neno lake kwao, na wanaochagua
kufuata dhambi za baba zao. Wale wamchukiao wamenaswa na kupotoshwa na dhambi
za baba yao, na dhambi hii na uasi inaweza kuwa matokeo na nguvu inayoongezeka
kwa kila kizazi kinachofuata na kinachochagua kumkataa - na kwa sababu hiyo,
bila mashaka watahukumiwa. Lakini mtu anaweza kugeuka kutoka dhambi za mababa
zake, na kama atafanya hivyo, Mungu anaweza kumsamehe dhambi zake na kumpokea
pasipo hata kuhitaji kutubu kwa ajili ya dhambi za mababa zake.
Lakini ni muhimu sana pia kutambua kwamba haisemwi kuwa Mungu huleta adhabu
au hukumu ya dhambi za baba kwa wana! Na Ezekiel 18 inathibitisha. Wana hawauchukui
uovu au adhabu ya dhambi za baba zao, isipokuwa kama wamechagua kuendelea katika
hizo. Wanapatilizwa dhambi za baba zao, ambacho ni kitu tofauti. Ni wazi kuwa
ikiwa mwana amelelewa na wazazi ambao wanatenda dhambi na kumwasi Bwana, hapo
mwana yu katika hatari ya mvuto wa maovu yao na baraka za Mungu hazipo katika
familia. Kwa hiyo dhambi ya wazazi inakuwa mtego kwa mtoto na bila shaka atajaribiwa
kufuata mfano mbaya, badala ya kumfuata Bwana. Kutoka 20 na Ezekiel 18 zinasimama
katika makubaliano kamili mmoja kwa mwingine katika kutoa kielelezo kwamba watoto
wanaweza kuvutwa vibaya na kunaswa na dhambi za baba zao. Lakini Mungu wakati
wote hutuchukulia kama mtu mmoja mmoja na humruhusu kila mmoja kufanya mwitikio
wake mwenyewe kwa Mungu. Kwa hiyo, hata kama dhambi za wazazi zitakuwa mtego
kwa watoto wao, bado wana uhuru wa kuchagua - wanaweza kuchagua kuziacha njia
mbovu za baba zao na kumgeukia Bwana. Hii imewekwa wazi na Ezekiel 18 na pia
na kusihi kwa Mungu akiwasihi Israel tena na tena katika vizazi vyao vinavyofuatana
waache uovu wao na uovu wa baba zao na kurudi kwake kwa moyo wao wote. Hakuwaacha
tu watu wake kwenye dhambi za baba zao. Alilitumia neno lake kwa kila kizazi
kupitia manabii wake, akiwataka watu wake wamrudie kuna mifano mingi ya jinsi
hii, kama Isaya 1:18,19. Tunaona pia jinsi ambavyo Asa, Hezekia au Yosia (2
Nyakati 14:29 na 34) walivyoacha dhambi za waliotangulia na kumrudia Mungu,
ndipo watu walipobarikiwa sana na Mungu. Uwepo wa Mungu ulikuwa pamoja nao tena,
na baraka na ulinzi wake. Na hakuna wakati tunapoona mmoja kati ya Wafalme hawa
kabla ya utawanyiko wakikiri dhambi za baba zao. Walitubu kwa ajili ya dhambi
zao wenyewe, ambazo bila shaka zingekuwa zilezile kama za baba zao - lakini
ilikuwa ni toba yao wenyewe tu ndiyo iliyotakiwa. Na walipofanya hivi, hapo
hapo na kwa wingi Mungu aliwasamehe na kuwabariki. Na haya yote yanaendana na
mstari 6 wa Kutoka 20 (ambapo tunaona kwamba rehema ya Mungu ni kuu mno kuliko
hukumu yake kwa wale wampendao na kumtii), na katika Ezekiel 18, ambapo tunaambiwa
kwamba mwana baada ya kufikiria njia mbaya za baba yake, anaweza kugeuka toka
uovu huo na kujinasua kutoka dhambi za baba yake anapomgeukia Bwana, ambaye
atawasamehe kabisa na asiwe na kinyongo chochote naye. Tunapozungumzia uhusiano
wa mtu na Mungu, Mungu haziweki dhambi za baba yake juu ya mtu huyo wala hamuadhibu
kwa ajili ya hizo! Mwana husamehewa na kubarikiwa pasipo kutubu kwa ajili ya
dhambi za baba yake! Waalimu hawa wa siku hizi wanataka tufungiwe ndani ya dhambi
za baba na wahenga wetu kwa njia ambayo hata katika Agano la kale haikujulikana,
na kwamba kwa hakika haina uhusiano na Agano jipya.
Sina budi kusema kwamba fungu la kutoka 20:4,5 lina vitu ambavyo si rahisi kuvielezea, na siwezi kusema kwamba nimeeleza kwa utimilifu. Lakini kwa kuwa Biblia ndicho kitabu peke yake chenye fafanuzi nzuri kuliko zote juu ya Biblia, tunapoliangalia fungu hili katika mwanga wa mafungu mengine, ingawa tutashindwa kueleza kwa utimilifu, bado kuna maandiko mengi ya kutosha ambayo yameangalia, kuona kwamba yale yanayofundishwa na hawa waandishi wa siku hizi, ni kitu ambacho hakifundishwi na neno la Mungu. Tafadhali rejea kwenye makala ihusuyo “Laana” kwa ajili ya mafindisho zaidi kuhusu sura hii ya Kutoka 20.
Msemo wa “dhambi ya kizazi” umebuniwa na waandishi hawa wa kisasa kwa ajili tu ya kuunga mkono mawazo yao ambayo si ya kibiblia. Msemo huo haumo ndani ya Biblia; huutumia kuunga mkono mawazo ambayo hayapatikani ndani ya Biblia. Ni kweli kwamba maisha maovu na mfano wa wazazi na jamii yanaweza kushawishi na kuathiri wengine ambao wanaendelea kukua, na kwa njia hiyo kama ambavyo ingesaidia kufanya mioyo yao iwe migumu kwa Injili. Hii ni kawaida na hakuna jipya. Lililo jipya, ni haya mafundisho yanayosema kwamba anapomgeukia Bwana, na pia kutubu dhambi zake, mtu au jamii inahitaji pia kutubu dhambi za baba zao au vizazi vilivyopita.
Wanatafuta “mifano” ya “dhambi za
vizazi” katika Agano jipya! Je, "uthibitisho" wa maandiko ni upi?
Wanadai ni Mathayo 23:32-35 na 1 Thesalonike 2:16! Hutuambia kuwa mistari hii
“huthibitisha" kuwa Agano Jipya hufundisha juu ya dhambi ya vizazi na kwa
sababu hiyo tunahitaji kutubu juu ya dhambi za vizazi vilivyopita! Mimi sidhani
hivyo. Mistari hii haitufundishi kwamba tunapaswa kutubu juu ya dhambi za wahenga
wetu! Wanarejea kwa wayahudi na jinsi wanavyochagua kupingana na Mungu. Swala
si kwamba wanalazimishwa kuendelea katika dhambi za baba zao, lakini ni kwamba
wanachagua kufanya hivyo. Hii ndiyo sababu Yesu aliulilia mji wa Yerusalemu.
Alikuwa anawategemea wampokee lakini wakachagua kutokumpokea. Hii inaweka msingi
wa hukumu yao isiyokwepeka. Mstari mwingine wanaounukuu kama uthibitisho ni
ule wa I Petro1:18. Lakini mstari huu wa ajabu unathibitisha kinyume na vile
wanavyofundisha. Mstari huu unatuambia kile ambacho nimekuwa nikisema katika
makala hii, kwamba damu ya Yesu Kristo, Mwana kondoo wa Mungu, ina uwezo kamili
na inatosha kutukomboa kutoka mwenendo wetu usiofaa tulioupokea kutoka nyuma
na kutoka mapokeo batili ya baba zetu. Tumekombolewa! Tumenunuliwa na kurudishwa
kwa damu ya Yesu. Hakuna tena hukumu ya adhabu juu yao walio katika Kristo Yesu.
Mungu Asifiwe! Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye
kuwahesabia haki! Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa;
naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea! (Rumi 8: 33,34).
Lakini mafundisho haya mapya yangetuletea hukumu sisi sote, yakituambia kuwa
si sisi wala jamii tunazoishi ndani yake tuko huru kikamilifu toka hukumu ya
Mungu mpaka hapo tunapokuwa tumetubu dhambi za baba zetu! Hili si jambo la kushangaza.
Kwa sababu kama ukimleta mtu chini ya sheria, mtu huyo hana budi kuwa chini
ya hukumu. Na hii ndiyo asili ya mafundisho haya.
Wanachanganya Kanisa na Ulimwengu
Ingawaje ni kitambo cha vizazi vingi, bado historia ya Waisrael inachukuliwa
kama ni Mungu alikuwa akishuhgulika na mtoto mmoja mmoja. Ni taifa moja pekee
na historia moja. (Kanisa ni mwili mmoja kiroho lakini linahusisha makanisa
madogo madogo ya aina nyingi katika maeneo mengi mbalimbali pamoja na watu wake,
wanaotokea katika mataifa mengi ya aina mbalimbali. Na hii bila shaka haishirikishi
historia ya aina moja au maendeleo ya kiroho, kama ilivyo katika Agano la Kale
- tazama nyaraka za Agano Jipya na Ufunuo sura 2-4.)
Sasa, ikiwa yeyote yule kama Akani (Joshua 7:1) au Sauli (2 Samweli 21:1) alifanya
dhambi, hii ingeweza kuleta madhara kwa wote, watu pamoja na baraka za Mungu
zingezuiliwa. Tena hayo mafundisho yao mapya yanasema, “Haya, unaona, kwa sababu
watu hawa walifanya dhambi, Mungu alizuia baraka zake hivyo tunahitaji kutubu
dhambi za nchi yetu!” Lakini kwanza, nchi yetu ipo mbinguni, na pili nyaraka
hizo hazitufundishi eti kanisa linapaswa kuungama na kutubu kwa ajili ya dhambi
za ulimwengu, kama vile nchi tunamoishi. Kinyume chake kwa urahisi tu, inamaanisha
tu kuwa, iwapo watu wa Mungu wakitenda dhambi watapata madhara katika maisha
yao au katika maisha ya kanisa (Rumi 8: 13, 1Kor 5:6, Ufunuo 2:5), na kama tulivyokwisha
tangulia kutaja hapo juu. Agano Jipya linatofautiana na Agano la Kale, ndani
yake kiasi kwamba, watu waliochaguo la Mungu katika Agano la Kale, wanawakilishwa
na taifa moja linalojulikana na historia yake ni moja wakati ambapo, kanisa
la Agano Jipya linahusika na watu wengi wa aina mbalimbali katika maeneo mengi
mbalimbali.
Hawa walimu wanataka kulinganisha na dhambi ya Akani - jinsi dhambi ya mtu mmoja
inavyoweza kuidhuru jumuia nzima. Akani alikuwa ni mmoja wa watu wa Mungu na
alifanya dhambi; dhambi yake iliwanyima waisraeli - watu wa Mungu - ulinzi wa
Mungu na baraka zake. Je, sasa wanataka kutufundisha kwamba, ikiwa mkristo atatenda
dhambi sehemu nyingine ya ulimwengu kwenye kanisa fulani, ndipo Mungu huzuia
baraka zake kwa wakristo wote ulimwengu mzima, hadi pale wote watakapogundua
nani aliyetenda dhambi hiyo, na kisha kanisa lote ulimwenguni kote litubu kwa
ajili ya dhambi ya mtu huyo? Kama ni hivyo basi, kanisa lote ulimwenguni kote
litahitaji kujua na kutubu kwa ajili ya dhambi alizokuwa akizitenda mkristo
mmoja mmoja au anazozitenda, kabla hatujaweza kuishi katika baraka zake Mungu.
Mpendwa msomaji unaweza ukaona wewe mwenyewe, matatizo yanayosababishwa na hayo
mafundisho yao, jinsi yanavyojaribu kupindisha maana ya maandiko ili kukidhi
mawazo yao.
Wanachanganya mafundisho ya Biblia yahusuyo kanisa na ulimwengu. Na wala haupo
mfano wowote katika Agano Jipya ambapo kanisa likiomba kwa vizazi vingine vilivyopita;
na wala haliwakilishwi na nchi yoyote iliyopo duniani. Kanisa linahusu Roho
iliyookolewa kutoka katika kila koo za makabila na mataifa.
Sasa katika makala hii nimekuwa nikitumia maneno mawili: “kuungama” na “kutubu”,
kwa sababu maneno hayo yote mawili yamekuwa yakitumiwa kwa uhuru sana katika
mafundisho haya ya kisasa kana kwamba yangeweza kutumika katika mazingira yale
yale, lakini mmoja wa waandishi wao wenyewe anakubali wazi wazi na kwa usahihi,
kwamba, hakuna njia yoyote ambayo watu wowote wa Agano la Kale kama vile Daniel
au Nehemia, kwamba wangeweza kutubu kwa ajili ya dhambi za vizazi vilivyopita.
Huwezi kutubia uovu wa aina yoyote ile ambao hujahusika nao. Kwa sababu toba
ni badiliko na kugeuka kutoka katika uovu ulioutenda. Kwa hiyo, ingawa je, Daniel
angeweza kutubu kwa ajili ya dhambi yoyote aliyoitenda, lakini yeye asingeweza
wala asingetubu kwa ajili ya dhambi za baba zake. Ndiyo, asingeweza, kwa sababu,
kwanza hazikuwa dhambi zake mwenyewe, (aliungama na kutubu kwa ajili ya dhambi
zake yeye mwenyewe, hata hivyo, dhambi za kumwasi Mungu hazikuwa zake). Na pili,
hakuna njia yoyote ile ambayo mtu yeyote anaweza kupokea msamaha toka kwa Mungu
kwa ajili ya watu ambao wamekufa. Hivyo kwa kweli ingeweza kuwa ni unajimu na
matendo ya tabia zisizo za ki-mungu.
Sasa, ijapokuwa walimu hawa wanaweza kukubali kuwa ni kweli, lakini bado katika
yote mawili, yaani ndani ya maandiko yao pamoja na mahubiri yao, wanazungumzia
kutubia dhambi za baba zetu, (jambo ambalo haliwezekaniki), au kuimwagia damu
ya Yesu katika dhambi za mji au taifa na hapo hapo eti upokee upatanisho kwa
ajili ya watu wa hapo (hii ni unajimu kama sio kufuru). Hakuna maombi yetu yoyote
ambayo yanaweza kusababisha msamaha toka kwa Mungu kwa ajili ya watu waishio
au waliokufa. Na bila shaka hatuwezi kuitumia damu ya mwokozi wetu kwa njia
ya jinsi hiyo. Damu yake Yesu sio aina fulani ya Hirizi.
Sasa yale ambayo bila shaka tunaweza kuona Daniel pamoja na wenzake wangeweza
kuyafanya ni kuumizwa juu ya dhambi za watu wa Mungu wanaomhusu. Upendo wake
kwa Mungu na kwa watu wa Mungu kwa kawaida ungeweza kumpelekea kuumizwa sana,
pale aonapo kwamba Waisrael wamemwasi Mungu, na kwamba watu wa Mungu wao wenyewe
wameondolewa utajiri wa baraka zake.
Isitoshe, ule ufahamu wetu wa umoja pamoja na watu wa Mungu, ungeweza kutupelekea
kuumizwa na kujinyenyekeza wenyewe mbele za Mungu, inapotokea kanisa haliishi
tena katika urithi wake ambao Kristo Yesu alinunua kwa ajili yetu pale Kalvari.
Badala ya kulihukumu kanisa, tunapaswa kujinyenyekeza wenyewe na kuiomba rehema
zake zitusaidie wakati wa uhitaji na kwa hakika hii inaweza pia ikajulisha kuungama
mambo mengine kama yalivyosababisha hitaji hili kubwa katikati yetu. Kwa kweli,
Roho wa Kristo atatuongoza katika hiyo (Rumi 8: 26,27, Efeso 6:19), lakini hii
haifanani kabisa na kutubu kwa ajili ya dhambi za wengine. Mtume Paulo aliwaombea
watakatifu (Wagalatia 4:19) bali yeye hakutubu kwa ajili ya dhambi zao. Alitafuta
Bwana kwa ajili yao, lakini baadaye alihakikisha wazi kabisa neno la kweli linawajia
ili kuwaongoza wamrudie Kristo.
Kwa hiyo tunaona kwamba, kuungama na kutubu kwa ajili vizazi vilivyopita hata
katika Agano la Kale, ili watu waweze kuzichukua baraka za wakati huo, hakufanywi
na watu wa Mungu kwa niaba ya watu wasioamini - katika miji au taifa. Halikadhalika,
aina hii ya maombi, hayakuwa na kawaida kwa watu wa Mungu, wanapozifikiria dhambi
zao wenyewe, bali aina hii ya maungamo ilikuwa inalingana tu na wakati wa kuondoshwa
kwa Waisrael na uahmishoni na inahusu Israel tu, kwa sababu ya agano zuri na
Historia yake nzuri ya matendo alivyojishughulisha nayo kwao kutokana na Agano
hili. Na pengine, lililo la maana zaidi ya yote, ni hili kwamba, aina hii ya
maungamo ya dhambi za vizazi vilivyopita yalifanyika kabla ya kifo na ufufuo
wa Kristo Yesu pale Kalvari, ambaye yeye pekee ndiye mpatanishi kati ya Mungu
na mwanadamu, kwa kuwa yeye ndiye amezichukua dhambi za wanadamu wote kwa yeyote
amwaminiye (1 Yoh 2:2).
Mafundisho haya mapya yanawakilisha kitu fulani cha tofauti kwa ukamilifu wa
Neema ya Mungu ambayo imeelezwa katika kumhubiri Kristo na kuwa yeye pekee ndiye
aliyesulubiwa.
Agano na Mataifa?
Kuna jambo lingine ambalo itakuwa ni vema ni kulielezea kutoka katika maandiko.
Tayari tumekwisha taja kuwa wangetutaka sisi tuamini kwamba, tunapaswa kuomba
kwa ajili ya miji na nchi tuishimo (ulimwengu) kama vile Daniel alivyofanya
kwa Israel (watu wa Mungu). Na kwamba Mungu alikuwa na maagano na mataifa ambayo
yaliruhusu aina hii ya maombi; wanawezaje basi, “kuruka” namna hii, toka kwa
watu wa Mungu hadi kwa watu wasioamini? Wao wananukuu mistari kama Kumb.32:8
ambao unasema kwamba Mungu, “… alipowapa mataifa urithi wao, alipobagua wanadamu…”,
na hii inarejea kwenye migawanyiko ya kijiografia katika dunia. Sasa haya mafundisho
mapya yanasema kuwa Mungu angeweza hayo tu kwa misingi ya agano la kisheria
na mataifa hayo na kwa hiyo wao pia walikuwa au wanaweza kuwa na uhusiano wa
Agano na Mungu kama Israel walivyofanya nyakati za agano la kale, na kwa hiyo
kanisa linaweza kuomba kwa ajili ya dhambi zilizopita na nchi wanayoishi? Inaonyesha
kuwa huu udanganyifu haufahamu mipaka ya upotoshaji wa kweli! Yesu Kristo alileta
jipya ili kuliondoa la kale (Heb. 7:12, 18,19,22; 8:13; 10:9). Lakini walimu
hao wanaanzisha maono ya kale yao wao wenyewe, na hatua yake inalichana jipya.
“Oho! Enyi wagalatia msio na akili, ni nani aliyewaloga?” Hayo yote kwa kweli
ni ubunifu wa ushirikina.
Tumekwisha ona kuwa maungamo ya Daniel yalihusu na uasi wa kurudiwa na Israel
kinyume na Mungu, kinyume na mafunuo yake, maalum ambayo aliwapa; pia ni kinyume
na agano ambalo alilifanya maalum kwa ajili yao kupitia Abrahamu na pale Sinai.
Agano hilo haliendi sambamba na taifa lolote katika maandiko. Mungu amepanga
na kuahidi zaidi na sio tu mgawanyiko wa urithi wa dunia hii. Kwa fadhili zake
Mungu amepanga kwa ajili ya wokovu wa watu wote watakaomwamini kutoka kwa taifa
au kabila la jinsi gani lolote lile watakalo. Hii ni uwazi wa ajabu kutoka katika
maandiko ya neno la Mungu na tunafurahia katika hilo kwa mioyo yetu yote! Lakini
hamna popote ambapo Mungu hata anapopataja, achilia mbali kuwataka, wakristo
au yoyete yule ahusike katika hatua za ushirikina huo wa kuungama au kutubu
kwa ajili ya dhambi za kitaifa za vizazi vilivyopita, kana kwamba hiyo inaweza
kutupatia baraka za Mungu na wokovu kwa ajili ya miji na nchi yetu.
Ni wazi kabisa kutoka katika Neno la Mungu, kwamba Mungu ametupatia baraka na
wokovu kwa watu wote kupitia kifo cha mwanae pale Kalvari. Tunaweza kuomba kwa
ajili ya kueneza Injili ili kwamba watu wapate kusikia ujumbe wa Kristo na kwamba
yeye kusulubiwa ili wapate kumgeukia toka katika dhambi zao, ambazo kwa uhuru
kabisa atawasaheme.
Ule mstari halisi ambao mwandishi wao mmojawapo anaunukuu, kutoka katika Kumb.
32:8 pia unanukuriwa na Paulo Mtume katika Matendo 17: 24-31 (mstari wa 26).
Hapa Paulo Mtume anaongea na watu wa Athene kuhusiana na ibada ya miungu yao.
Hawaambii kuwa laana ya Mungu iko juu yao kwa sababu ya Kutoka 20:5, na kwamba
wanapaswa kutubu kwa ajili ya ibada ya miungu yao uliopita kabla ya kubarikiwa
na Mungu. Hapana, hasemi hivyo, isipokuwa anawaambia kuwa Mungu aliweka mipaka
ya nchi yao ili kwamba watu wapate kumtafuta Bwana (mstari wa 27). Hauelezi
chochote kuhusu uhusiano wa agano kutoka katika agano la kale, ambalo sasa linawahitaji
wao watubu dhambi zao nyingi zilizopita za miji na nchi ya Athen, vita vyake,
na ibada ya sanamu yake! Hapana! Isipokuwa yeye badala yake anawaambia kuwa,
Mungu alifanya kama haoni katika enzi za ujinga wao, lakini sasa anawaagiza
watu wote watubu. Ndipo anaanza kuwaelezea kuhusu Yesu na ufufuo wake.
Inafanana pia na katika Matendo 14:16, ambapo watu wa Listra walitaka kumtolea
dhabihu Paulo na Barnaba, wala Paulo hakuwakaripia na kuwaambia kuwa walikuwa
chini ya laana ya Mungu, kwa sababu ya ibada ya sanamu yao mbaya na hivyo walitakiwa
watubu dhambi za mababa zao kwanza, kabla Mungu hajawabariki wao bali pamoja
na nchi yao; Hapana! Aliwaambia kuwa yeye alikuwa ni mtu kama wao, na kwa uwazi
kabisa lakini kwa fadhili aliwahitaji wageuke na kuyaacha mambo hayo ya ubatili
wamrudie na kumwelekea Mungu aliyehai, ambaye Mtume Paulo anasema “….ambaye
zamani zilizopita aliwaacha mataifa yote waende katika njia zao wenyewe, lakini
hakujiacha pasipo ushuhuda; kwa kuwa alitenda mema akiwapa mvua kutoka mbinguni,
akiwashibisha mioyo yenu chakula na furaha…”. Hii ingeweza kuwa ni fursa ya
pekee kwa Mtume Paulo kuweza kuhalalisha mafundisho haya mapya; lakini badala
yake, hafanyi chochote cha aina hiyo, wala hazunguki huko na huko akihubiri
laana na hukumu kwa sababu ya dhambi za vizazi ambavyo watu wanahitaji kuungamia
na kutubuia; mpendwa msomaji wangu; tafadhali angalia jinsi ambavyo maandiko
ya Neno la Mungu yanavyowakilisha karibu ni kinyume kabisa cha picha halisi
ya yale mafundisho wanayoyatengeneza wao.
Katika mipangilio ya kuhubiri Injili, Mungu haweki majukumu yoyote juu ya taifa
kwa ajili ya dhambi za vizazi vilivyopita (Rumi 3:24). Kwa kweli Mtume Paulo
anasema, Mungu alifanya kama haoni katika nyakati zao za ujinga, ni vema kuliko
kuongelea kuhusu ujumla wa mibaraka za Mungu ambazo kwa fadhili zake Mungu ameendelea
kuzitoa chini ya nyakati zote kwa watu wote.
Na hii haishangazi kwa sababu kinyume na hayo mafundisho yao mapya, Mungu hajajifunua
mwenyewe kwa namna ya pekee kwa mataifa kabla ya Kristo, kama alivyofanya kwa
Israel. Hajafunua kwa mataifa haki yake na tabia yake takatifu kupitia sheria
zake za manabii, na alijitokeza kwa mafunuo maalum. Hajalianzisha agano pamoja
nao, ambalo kwa hilo sasa aweza kuwahukumia. Hapana, mbali ya kutambua uasili
ambao unapaswa kuwa ndani ya moyo wa mume na mwanamke, kumhusu Bwana wao (Rumi
1: 19,20), kimsingi, walikuwa hawajapata mafunuo maalum kuhusiana na tabia ya
haki yake na matakwa ya haki yake; na kwa hiyo Mungu kwa ujumla alikuwa hawakabi
kuhusika na yaliyopita (yeye aliyepewa machache, machache yatahitajika) kinyume
chake, anaendelea kuwa mwema kwao na anawabariki. Lakini kama Mtume Paulo alivyosema,
sasa anawaagiza wote watubu dhambi zao wao wenyewe, na kumrudia Mungu aliye
hai! Haleluya! Hii ndiyo Injili!
Mstari maalum wanaoutumia ili kufunga mkono mafundisho (Kumb. 32:8), unanukuliwa
na kuelezwa na Mtume Paulo, kufundisha kinyume cha mawazo yao!
Wanasema unapaswa kuungama na kutubu kwa ajili ya dhambi za “nchi yako” kwa
sababu eti ya uhusiano wa Agano (!?) kati ya Mungu na nchi ile, kabla Mungu
kwa hakika hajakubariki wewe na nchi yako. Mtume Paulo anasema kuwa, Mungu alijua
kuwa mataifa yalikuwa katika ujinga kwa tabia yake na haki, na kwa hiyo katika
wema wake na rehema yake alifanya kama haoni, zilikuwa ni kama vizuri kwao,
lakini kwa sasa anawaagiza wote kutubu, kwa sababu ya wokovu unaotolewa katika
Kristo Yesu!
Hii ndiyo neema, maajabu na wepesi wa Injili. Hebu tuipokee hazina hii, tuitunze
na kuitangaza.
Sasa tunaweza kuona jinsi wanavyofanya makosa makubwa. Msingi halisi wa mafundisho
yao umesimikwa juu ya makosa ya kuwabadilisha au kuwachanganya watu wa Mungu
na wasioamini. Wanawajali wenye dhambi na wasioamini kana kwamba ni watu wa
Mungu waishio chini ya Agano la Kale – ambapo kanisa linapaswa kuomba kwa ajili
ya ulimwengu kama vile Danieli alivyofanya kwa ajili ya Waisraeli! Kwa hiyo
wanatenda makosa mawili makubwa na ya kumsingi. Kwanza, wasioamini sio watu
wa Mungu waliokombolewa na hawawezi kutendewa au kuhesabiwa kama hivyo katika
mahubiri au kuomba (ijapokuwa kwa vyo vyote vile tunapaswa kuomba na kuihubiri
Injili kwao). Jambo la pili, Yesu Kristo alipokufa pale Kalvari alilia “Imekwisha!”
Hii ililijumlisha na Agano la Kale. Imekwisha, kwa kuwa Kristo ametukomboa kutokana
na sheria (Rum 7:6). Torati na manabii vilikuwapo mpaka kipindi cha Yohana,
lakini sasa Ufalme wa Mungu unahubiriwa (Mt 11:12,13; Luka 16:16) au angalau
ingekuwa hivi. Hatupo chini ya Agano la Kale tena, lakini hapo ndipo wangependa
kutuweka sisi kama wangeweza kufanya hivyo! Mbaya zaidi, yale wanayoyafundisha
ni mtindo wa uchafu wa Agano la Kale. Tumekwisha kuona jinsi ambavyo mafundisho
yao yote yalivyo; yanapatikana kutokana na tafsiri yao wenyewe ya kitabu cha
Kutoka 20:3-5 na Walawi 26:40. Je huo ni ufunuo wa Agano Jipya? Hapana!
SEHEMU YA PILI
Tukiangalia kwa makini maandiko yasemavyo:
Injili
Kama vile ilivyokuwa huko Galatia, vivyo hivyo leo mafundisho ya aina hii yanapora
mahubiri ya Msalaba, uweza wake na utimilifu wake. Hii ni kasoro ya aina ya
kizamani sana ni ya kienyeji. Inapotosha ukweli wa Injili, na inaturudisha nyuma
hadi kwenye mtazamo wa aina ya Agano la Kale; wakielezea kwa jinsi hiyo, kwa
uhakika, inawakilisha mashambulizi dhidi ya Injili ya Kristo na kile alichokipata
pale Kalvari. Inatuondolea mtazamo wetu mbali na Kristo na inalikuza Agano la
Kale. Hali kadhalika inafunua ukosefu wa ufahamu wa kile kilichomo ndani ya
Agano Jipya. Ili kuonyesha kuwa hivyo ndivyo ilivyo, litakuwa ni jambo la faida
kwetu sasa iwapo tutayatazama maandiko yanasema nini juu ya baadhi ya mambo
haya. Tumekwisha onyesha wazi kuwa Agano Jipya halina hata mfano mmoja wa aina
hii mpya ya mafundisho.
Hebu basi tuone katika Agano Jipya linatufundisha nini katika 2 Kor 5:19, tumesoma
kuwa,
“…Mungu alikuwa ndani ya Kristo, akiupatanisha ulimwengu na nafsi yake, asiwahesabie
makosa yao…”
Warumi 5:8 inasema, “...bali Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi,
kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu tulipokuwa tungali wenye dhambi.”
Waefeso 2:11 nayo inatuambia, “…akawapatanisha wote wawili na Mungu, katika
mwili mmoja kwa msalaba, akishaufisha ule uadui kwa huo msalaba. Akaja akahubiri
amani kwenu ninyi mliokuwa mbali, na amani kwao wale waliokuwa karibu.”
Hii ni mistari ya thamani na ya muhimu, kwa sababu inafunua moyo halisi wa Injili,
msingi wa wokovu wetu na neema ya Mungu ya ajabu kwetu sisi katika Kristo Yesu.
Tulipokuwa bado tungali wenye dhambi, kabla hata hatujaweza kufikiria juu ya
Mungu au kujali juu yake au hata juu ya amri zake, kabla hatuja mkaribisha kwa
njia yoyote ile; yeye mwenyewe Mungu Baba, kupitia mwanawe Yesu, alikusudia
kutujia na kwa niaba yetu kupokea msamaha wa dhambi hizo katika maisha yetu
na kuziondoa hukumu zake juu ya maisha yetu kwa ajili ya hizo dhambi zilizopita,
(Rumi: 3:24-28). Hivyo ndivyo alivyofanya pale Kalvari. Pasipo gharama yoyote
alizichukua dhambi zetu na kuziharibu nguvu zake. Hili halikuwa tu ni wazo la
baadae isipokuwa hayo yote yalitokea kulingana na kusudi lake la milele na kufurahishwa
kwema kwa nia yake. Mungu asifiwe!
Mungu alitimiza yote kwa niaba yetu pasipo hata kutaka tulipe gharama (ni bure).
Ni kwa neema, na kwa sababu ya neema ya Mungu, watu wanasamehewa na kuokolewa.
Ilifanywa kwa ajli yao, hata walikuwa wafu katika makosa na dhambi, (Efeso 2:4-9).
Na sasa Mungu huwapa haki watu wasio wanyofu kwa imani peke yake (Rumi 5: 4,5).
Na pasipo hata kujitahidi kwa watakatifu wenyewe ili kujaribu kupata msamaha
na upatanisho kwa ajili ya wenye dhambi, miji au Taifa; kwa kutubu kwa ajili
ya dhambi zao. Kwa maneno mengine, pasipo hata kuwataka watakatifu kuongezea
chochote kile juu ya neema na kazi za Mungu aliyoipata pale Kalvari kupitia
Kristo!
Tumekombolewa kutoka katika mwenendo usiofaa ambao tuliupokea kutokana na mila
na desturi za mababa zetu, kupitia damu ya thamani yaa Yesu Kristo; hapa sio
kwa kupitia maombi ya watakatifu wala maungamo yao, (1 Petro 1:18,19). Hatuoni
haja yoyote ya kuendelea kuzichambua dhambi zilizopita, yaani za mababa zetu
ili kwamba sisi tupate kupokea wokovu huu kamili na ili tupate kuwa huru kabisa!
Ni nini au ni nani atakayetuhukumu, atakayetushitaki, au kutuweka katika vifungo?
Je, ni dhambi za mababa zetu? Hapana! Damu ya Kristo imetukomboa! Kwa maana
damu ya Kristo imetufaa kabisa na ni kwa wakati wote; na wokovu wake upo wazi
na ni kamili kwa yeyote atakayetubu na kuamini. Baadhi ya hao walimu wao wa
kisasa wanasema kuwa, eti mstari huu unaopatikana katika Petro wa kwanza unathibitisha
mawazo ya dhambi za vizazi, na kwamba, kwa hiyo sisi twapaswa kuungama na kutubu
kwa ajili ya dhambi hizo za mababa zetu! Lakini katika sura ile, Petro hawaelekezi
kufanya jambo lolote la aina ya mawazo yao hayo. Ni wapi basi anapokazia hitimisho
lake, kwamba tunapaswa kuomba kwa ajili ya hilo, na kutubu kwa ajili ya dhambi
za mababa zetu? Kwa hakika, hapo anatufundisha kinyume kabisa cha dhana ya mapokeo
yao. Yaani, hapo anatufundisha kwamba, damu ya Kristo imefanya kazi yake, ametukomboa
sisi kutokana na mila na desturi za mababa zetu. Kwa hiyo, mapokeo na maelekezo
yao, kwa hakika ni mapokeo yanayoendeleza mashambulizi juu ya utimilifu wa uhuru
ambao Mungu ameutoa katika huyo Kristo kwa ajili ya wanaume na wanawake wote.
Ukweli huu, uhusuo wokovu wetu kamili unafafanuliwa vizuri zaidi katika Warumi
5:15-21, ambapo tunasoma kwamba, dhambi na hukumu iliyowajilia watu wote kwa
sababu ya Adamu wa kwanza, sasa kwa Kristo ambaye ndiye Adamu wa pili ametuondolea
pasipo malipo yoyote; bali ni kwa kifo chake pale Kalvari, akitupatia msamaha
na haki kwa wote watakaomwamini. Kwa maneno mengine, tungeweza kusema kuwa dhambi
zao zote zisingeweza kuwashikilia kwa kuwa Kristo amewaondoa mzigo wa uwajibikaji
kwa ajili ya hilo, kama vile Isaya anavyotutaarifu, katika ile sura ya 53. Na
hii ndiyo maana halisi ya 2 Kor 5:19.
Hii ni habari njema ya Injili na sasa wanaume kwa wanawake wanaitwa ili kuziamini
habari njema hizi na kugeuka kutoka katika dhambi zao. Imani hii ndiyo wokovu
wao; kwa sababu hiyo tunasoma kwamba, Mungu alikuwa ndani ya Kristo, asiwahesabie
makosa yao (kwa vile yeye mwenyewe angeyaondoa). Kwa hiyo, Yesu alimwambia mtu
yule aliyepooza ambaye alipelekwa kwake kwa ajili ya kuponywa, (kama ilivyo
katika Injili ya Luka 5), kwamba, dhambi zake zimesamehewa pasipo malipo (bure)
kwa sababu tu aliamini. Katika Injili ya Yohana sura 8 anamwambia mwanamke aliyefumaniwa
katika uzinzi, kwamba, hamhukumu, isipokuwa aende zake na asifanye dhambi tena.
Katika Injili ya Yohana 4, anatoa maji ya wokovu bure kwa mwanamke Msamaria
- kwa hakika msamaha sasa uilikuwa ni bure, na Mungu mwenyewe alikuwa akipatanisha
wanaume na wanawake na nafsi yake mwenyewe. Kwa sababu alikuwa akienda kuliondoa
lile pingamizi kuu la dhambi, ambalo limewashikilia watu wote katika vifungo
vya dhambi na mauti; kuanzia wakati ule wa Adamu. Misingi yote ya mambo ilikuwa
inaenda kubadilika kwa sababu ya Kalvari - “... kwa maana manabii wote na torati
walitabiri mpaka wakati wa Yohana…”, Mathayo 11:13. Katika Luka 13:1-5, Yesu
analiweka wazi zaidi kwa hao anaoongea nao, kwamba hawapo watu wengine ambao
wao ni watenda dhambi wakubwa kuliko wengine; bali wote wamekufa katika makosa
na dhambi; hata kama kwa nje wanaonekana wanatenda dhambi nyingi au kidogo;
hapo hakuna tofauti, hali ya kila mmoja wao ni (Rumi 3:10,12,23). Sio wingi
wa yale wanayoyafanya watu, isipokuwa ni ile hali yao. Hali ya watu wote (wanaume
kwa wanawake) ni moja, ni ya dhambi na kifo na kutengwa kutoka kwa Mungu. Jambo
hili halikufunuliwa kwa uwazi zaidi ndani ya Agano la Kale, kwa sababu hapakuwepo
na matengenezo kwa ajili ya hali hii ya dhambi katika wakati ule. (Gal.3:22-25
; 4:3-5; Rumi 3:19-22; Heb 1:1-2 ; 9:6,9 ; 10:1 ; 4:9,10). Lakini kwa sasa,
kutokana na kujidhihirisha kwa Yesu, ukaja ufunuo wa kudumu, wenye kina cha
uozo wa mwanadamu, kwa sababu, Mungu sasa alikuwa akitoa matengenezo kamili
juu ya hali hiyo na alikuwa akifanya hivyo bure nje ya upendo na neema yake
isiyo na ukomo.
Yesu hakuja kuwahukumu kwa ajili ya dhambi zao ambazo alipaswa kufa kwa ajili
ya hizo (Yohana 3:17; 12:4), bali kuwapatia wokovu bure wale wote watakaotubu
na kuamini Injili. Hii ndiyo maana halisi ya ile mistari mikuu inayopatikana
katika Yoh. 3:16 –18. Mungu alifahamu wazi kuwa watu wote walikuwa katika vifungo
kwa dhambi na kwamba kifo kilitawala ndani yao kwa sababu ya dhambi. Alikuwa
hawalaumu kwa jambo hilo kwa maana hayo yote yalikuwa ni matokeo ya dhambi ya
Adamu, na yeye Yesu, alikuwa anaenda kuzibeba dhambi hizo zote pamoja na hukumu
zake pale Kalvari. Kuendelea kung’ang’ania juu ya dhambi moja na kuukataa msaada
wa bure wa msamaha na wokovu; jambo hili linawakilisha dhambi ambazo watu watahukumiwa
nazo.
Kile ambacho kinafanywa na mafundisho hayo yao mapya ni kuzifufua dhambi zile ambazo Yesu alikwisha mwaga damu yake kwa ajili ya hizo, na wakati huo huo kuwataka watakatifu kuomba kwa ajili ya dhambi hizo! Walimu hao wa kisasa wangekataa hizo; lakini wao hawajali madhara ya mafundisho yao. Hii inatoa mifano pia ya jinsi wanavyotumia vibaya ile 2 Kor 5:19. Wao wanasema kuwa, huduma hii ya upatanisho ni sehemu muhimu ya huduma ya kanisa.
Ndiyo, kwa kweli ni sawa, lakini je, maana yao hasa ni nini? Wanaharibu maana halisi ya sura hiyo; pale wanaposema kuwa ni sehemu ya huduma ya kanisa, kuupatanisha ulimwengu (mji, au nchi inayotuhusu) kwa Mungu! Na ni kwa jinsi gani basi? Kwa kuungama na kutubu dhambi za Nchi “yetu” na kujitwalia damu ya Yesu kwa dhambi hizo? Lakini maana hii waitoayo, hatupewi popote pale na Mtume Paulo! Hasemi kuwa Mungu yupo katika kanisa na akiwaongoza watakatifu leo kuungama na kutubu kwa ajili ya dhambi za jumuia ili kwamba apate kuwasamehe! Isipokuwa yeye anasema kuwa, Mungu alikuwa ndani ya Kristo na katika huyo Kristo alikuwa akiupatanisha ulimwengu na yeye mwenyewe asiwahesabie makosa yao; sasa kwa nini kuzifufua dhambi ambazo Mungu hazihesabii kwa ulimwengu? Ili kwamba eti kanisa liweze kutubu na kuungama kwa ajili hizo? Huu ni utata na mkanganyiko mkubwa! Katika sura hiyo yote tokea ule mstari wa 14 mpaka wa 21 kimsingi inaelezwa yale ambayo Mungu aliyafanya kupitia Kristo pale Kalvari kwa niaba ya wanadamu. Imefanywa! Mungu amefanya! Imekwisha na wala hakuna yeyote awezaye kuongezea lolote lile juu ya hilo!
Katika ule mstari wa 18 anatuambia kuwa Mungu alitupatanisha na yeye mwenyewe kupitia mwanae Yesu Kristo; wala kamwe haikuwa ni kanisa lililofanya hilo kwa kupitia maombi ya kuungama na kutubu! Mafundisho hayo yanajaribu kuongeza au kupunguza utimilifu wa Kalvari kupitia ubunifu wa hizi kazi zao za upatanisho, ambazo kanisa lililazimika kutimiliza kupitia kile wanachokiita wao maombezi ya utambulisho. Lakini Paulo haungami wala kutubu kwa ajili ya dhambi za yeyote yule katika waraka huu! Hii ni nini basi “Neno” au “huduma ya neno ya upatanisho” ile ambayo mtume Paulo ameitaja katika mstari ule wa 18,19? Ni sawa kuwa anatuambia sisi, “…naye alitupa huduma ya upatanisho yaani, Mungu alikuwa ndani ya Kristo akiupatanisha ulimwengu na nafsi yake asiwahesabie makosa yao”. Tangazo la ujumbe huu ni “Neno”au “huduma ya upatanisho” - kutangaza kwa watu kile ambacho Mungu amekifanya katika Kristo kwa niaba yao, ni ujumbe wa neema uletao amani, kuwa upatanisho wanaume kwa wanawake kwa Mungu. Tazama kwa makini kile ambacho Paulo amekifanya ndani ya waraka huu, tunaona kuwa hajaribu kupata upatanisho kwa ajili ya tabia za kimwili walizo nazo wakorintho kwa kupitia maombi ya toba kwa niaba yao.
Tunamwona Mtume Paulo akitangaza
kwa wakorintho kile ambacho Mungu amekwisha kifanya ndani ya Kristo kwa niaba
yao, na ili baadae waweze kuelewa kuwa yawapasa kuwa ni watu wa aina gani katika
hali ya ukweli huu wenye utukufu; ndipo sasa anawaagiza kupatana na Mungu, “…kana
kwamba Mungu alikuwa akiwasihi (sio kuomba maombi ya toba kupitia kwetu sisi)….tunawasihi
……mpatanishwe na Mungu”. Ametangaza neno la Mungu lenye neema kwao ili kwamba
ikibidi wapate kurejea na kutubu.
Hebu basi tuangalie kwa ufasaha zaidi jambo hili. Ni kweli kwamba unaweza kuhuzunishwa
hadi kufikia kutoka machozi na maumivu ndani ya maombi, pale tuonapo ndugu zetu
wakitenda dhambi au wakienda mbali na Mungu, 2 Kor 2:4; Gal 4:19; kwa ujumla
tunapaswa kuguswa na mambo yale yanayoumiza mwili wa Kristo na hivyo kuombeana
mbele ya kiti cha enzi cha neema ya Mungu na wema wake upate kuwaongoza wale
waliofanya dhambi wapate kutubu na kwamba rehema zake zipate kurejesha tena
mioyo yao kwake. Lakini sasa, jambo hili lipo tofauti kabisa na hayo mafundisho
yao ya kisasa. Wao wanatusihi tuyafanye yale wanayotufundisha, kwamba wanatutaka
tutubu kwa ajili ya dhambi za dunia, yaani, dhambi za watu wasioamini! Lakini
kwa chochote kile tunachoweza kuombea, tusisahau kabisa kwamba yupo mpatanishi
mmoja tu kati ya Mungu na wanadamu, na huyo ndiye mwanadamu Yesu Kristo; na
sasa hayo mafundisho yao ya kisasa yanapoteza mwelekeo wao katika ukweli huu.
Tunaliona hili mara nyingi katika
Biblia kwamba neno la kweli la Mungu huja kwa mtu binafsi likimtaka kugeuka
toka dhambini kwenda kwa yeye; na katika Agano Jipya hili ni neno lenye utukufu,
limejaa neema na kweli, likiwataka waume kwa wake wokovu wa bure katika Kristo.
Dhambi zao zilizopita haziwezi kuwatenga wala kuwazuia katika kupokea wokovu.
Mungu hawahesabii tena dhambi hizo zilizopita ndani yao (kwa sababu ya Kalvari).
Lakini kwa hakika sehemu ya wokovu huu mkuu ni kwamba, watu wanapokea msamaha
wa dhambi zao zote zilizopita kupitia damu ya Kristo, pale tu wanapokea habari
hii ya upatanisho.
(Rumi10:9-10, ukisoma kwa makini katika mistari hiyo, utaona kuwa Mungu anamtaka
mtu binafsi amwamini Yesu na kumpokea moyoni mwake ili aweze kuokolewa; na wala
si vinginevyo).
Lakini ili kuendelea na ujumbe wetu; tatizo halisi hapa sio kwamba watu wanafanya wizi, kuua n.k. bali tatizo ni kwamba, kuhukumiwa kwao ni kuwa mtu haiamini habari njema na hachukui hatua ya kuondoka kutoka katika giza. Katika Injili ya Yohana 16:9 tunasoma kwamba, hivyo Roho Mtakatifu atakapokuja atauhakikishia ulimwengu kwa habari ya dhambi. Sasa ni jambo la maana sana kugundua na kuelewa kuwa, ni kwa nini auhakikishie ulimwengu kwa habari ya dhambi?
Kwa hatua ya kwanza, haiwi hivyo kwa sababu ya kudanganya, kuiba, uchawi, uzinzi na kuua, bali Roho Mtakatifu atawashawishi juu ya dhambi kwa sababu hawakuamini. Hivyo ndiyo sababu ya msingi inayowazuia watu kuokoka - kule kutokuamini kwao. Ufahamu kuwa, Kalvari imekwishaishughulikia dhambi pamoja na nguvu yake. Waache watu sasa watubu na kuamini Injili. Mafundisho hayo yahusuyo kutubu kwa ajili ya dhambi za wenye dhambi, yanashambulia na kudhalilisha ukweli - iwapo mtu atakuwa amejihusisha katika uchafu, ulevi au uchawi, atahitaji pia kupata ukombozi maalumu ili kuondokana na mambo hayo; katika namna ambayo sio lazima wote waipitie hiyo. Mambo hayo yanaweza na yanafanya madhara makubwa na uharibifu katika maisha ya mtu iwapo atayaendea na kuyafanya. Lakini jawabu la hilo sio, kwa wengine kuanza kutubu kwa ajili ya dhambi za hao, badala yake ni kuomba, kwa mfano, mlango wa kuingia Injili upate kufunguliwa kwa ajili ya watu hao - hilo tu linalotupasa kufanya kwa ajili yao.
Katika Agano Jipya tatizo kubwa lililokuwepo la kueneza na kuipokea Injili, haionyeshi kuwa ni “dhambi” ya watu, dhambi zile wanazozitenda watu! Isipokuwa ni kule kutokuamini kwao. Katika Injili, tunaona kuwa, ilikuwa ni watenda dhambi ndio waaliokuwa wakimiminika kwenda kwa Yesu: wanyang’anyi, makahaba, watu wachafu na wale waliopagawa na mapepo; na wala sio watu wenye dini; hawa watu walikuwa ndio wale ambao hawakumuamini! Ndani ya mji wake mwenyewe, Yesu hakuweza kabisa kufanya miujiza mingi, sio kwa sababu ya uovu wa mji ule, isipokuwa ni kwa sababu ya kutokuamini kwao (Mty 13:58).
Tunaona pia katika Matendo ya Mitume, kwamba, kimsingi haikuwa ni kwa sababu ya dhambi za watu kama vile uchawi wao, ulevi wao na uuaji, ambavyo viliwakilisha kuzuiwa kwa Injili. Kwa mapenzi ya Mungu mwenyewe, Mtume Paulo na wengineo walitembea moja kwa moja katika mazingira ya miji ya jinsi hiyo, kama vile mji wa Samaria na Efeso, na Mungu alifanya kazi ya ajabu huko (wala pasipo hata kuomba au kuhubiri kwamba mmoja anapaswa kutubu kwanza kwa ajili ya dhambi za mji ule). Tatizo lililokuwa hapo ni kutokuamini, ugumu wa mioyo kuelekea ukweli, mara nyingi kutoka kwa watu wa dini; haijalishi kama wao walikuwa ni Wayahudi au kutoka kwa hao waliojishughulisha na kuabudu sanamu. Unapoendelea kusoma Matendo ya Mitume utagundua kuwa tatizo halikuwa ni dhambi ya watu, isipokuwa ni ugumu wa mioyo yao kuelekea ukweli - kutokuamini (kwa ajili ya sababu yoyote ile iwayo). Ndilo litakalo wahukumu watu siku hiyo, sawasawa na kazi zao kama maandiko ya Neno la Mungu yaonyeshavyo - kwa uwazi sana; na watu wanapaswa kuambiwa hayo. Lakini kwa mujibu wa tangazo la Injili tunapaswa kuanza kueleza kwa watu wote ule msamaha wa Mungu utolewao bure kwa njia ya Kristo ambaye alifufuliwa kutoka kwa wafu kwa ajili ya haki yao. Kutokuamini na kutokupokea. Hiyo ndiyo dhambi ya wanadamu.
Katika uwazi wa ukweli huu wote na ufunuo, mitume wangewezaje basi kutubu au kuwaambia wengine ili watubu kwa ajili ya dhambi za wasioamini katika nchi na miji yao? Yesu Kristo tayari alikwishawafia kwa ajili ya dhambi zao, na amekwisha lipa bei ya upatanisho wao (1Yoh.1:2)! Msamaha wa wokovu tayari umekwisha patikana katika Kristo, watu wanapaswa sasa kuamini habari njema, na wao wenyewe, yaani wao binafsi, ndio wenye dhambi zao. Kristo aliteswa mara moja kwa ajili ya dhambi, na sasa je, tunafikiria kuongelea chochote juu ya kazi yake aliyoimaliza kwa kutubu kwa ajili ya dhambi hizo mbele za Mungu na kuomba msamaha kwa damu ya Yesu Kristo –wakati ambapo damu yake iliyomwagika pale Kalvari tayari imepokeo hayo?
Je, mateso yetu tunayo yapata tuombapo na kutubu yanaweza kutupatia msamaha zaidi kwa ajili ya wenye dhambi? Au tunadhani kuwa toba yetu kwa ajili ya dhambi zao kwa namna nyingine, labda sasa inamwezesha Mungu kuibariki mikoa na miji yetu pamoja na watu wake kwa Injili? (Watu wanaweza kudhani kuwa wao ni kama Daniel, wafanyapo hayo, lakini kwa masikitiko makubwa na kwa ubaya zaidi wamekosea). Ni nini? Mungu aliwasamehe waume kwa wake bure pale Kalvari; kisha eti watakatifu watubu kwa ajili dhambi hizo hizo ndani ya maombi yao ili kwamba Mungu apate kuwasamehe na matendo yao maovu? (Afanye hivyo kwa mara nyingine tena?). Na kwamba hii eti imzuie Mungu kuibariki miji au mikoa ili kwamba wenye dhambi wenyewe wapate tena kuzitubia dhambi hizo hizo na kupokea msamaha pia. (Je, mara nyingine tena?). Ni mchanganyiko wa jinsi gani huu? Ni aina gani ya mchanganyiko wa mawazo yasiyo na afya ya Agano la Kale na Jipya, ambayo yanaweza tu kuwadanganya watu kuhusiana na ukweli? Linaloshangaza zaidi, ni ule ukweli kuwa baadhi ya wahubiri wanasafiri huko na huko katika miji na kuhubiri hadharani kwa watakatifu pamoja na wenye dhambi, wakiwaeleza kwamba ni lazima watubu kwa ajili ya dhambi za nchi zao badala ya kuwapatia ukweli wa Injili wale wasioamini - kuwapa pia ujumbe wa Kristo na kwamba yeye ndiye aliyesulubiwa, kwamba Kristo alikufa na amefufuka kutoka kwa wafu na ameziondoa dhambi zetu zote, kwa ajili ya kutupatia msamaha na haki!
Wanatujia kwa mtindo wa baadhi ya manabii wa Agano la Kale, kama vile Yona au Yeremia wakiitangaza hukumu ya Mungu juu ya Taifa kwa ajili ya dhambi zake; wakati ambapo tumekwishaelezwa kwa uwazi kabisa kuwa nyakati za zamani Mungu aliongea na baba zetu kwa vinywa vya manabii; nyakati hizi za mwisho ameongea nasi kwa njia ya Mwana wake. Waebr.1:1,2. Sio tu kwamba Mungu amemchagua Mtu wa tofauti kabisa na wapokee mtu halisi wa kutuunganisha; bali ni kwamba ujumbe na huduma sasa ni mpya kabisa kwa sababu ya Mtu mwenyewe aliyechaguliwa na Mungu - Yesu Kristo, na kile alichokwisha kukifanya! Torati ilitolewa na Musa, lakini neema na kweli zilikuja kwa njia ya Kristo Yesu. Lakini hawa wahubiri wengineo wanahubiri kitu cha tofauti kabisa, na kitu kingine ambacho kipo jirani kabisa na torati na hukumu kuliko Injili na neema. Hata kama katika suala la Yona, yeye aliwaambia watu wa Ninawi wao wenyewe watubu, (wao binafsi). Hakuwataka kutubu kwa ajili ya dhambi za watu wengine katika mji ule! Na bila shaka Yona hakutubu kwa ajili ya dhambi zao.
Hebu niseme hapa, kwa vyovyote vile tunaweza na pengine tumehuzunishwa na yale yanayoendelea kufanyika katika jamii zetu au jamii na kwa hiyo tunaweza kuomba kuhusiana na vitu vya namna hiyo ambavyo ni vya wazi na vinavyotuhuzunisha na ambavyo vinaweza kutumika pia kama vizuizi vya watu kuisikia na kuipoke Injili. Na kwa hakika, tunaweza pengine kufikiri kuwa mambo yameenda mbali zaidi kiasi kwamba tunafikia hatua inayoonyesha kuiva kwa hukumu ya mwisho ya Mungu juu ya dunia. Na kwa hivyo, hiyo inaweza kutushurutisha kuomba kwa bidii sana, kwa ajili ya hali na huduma ya kanisa kwa ulimwengu huu uliopotea na wenye machukizo, hivyo kutangaza kwa bidii haja ya waume kwa wake kutubu. Hata hivyo, hiyo nayo tena hailingani kabisa na haya makubaliano ya kisasa yanayopenda kututaka sisi tufanye; katika kutubu kwa ajiliya dhambi za ulimwengu na katika jamii yenye kushutumiwa kama baadhi ya manabii wa Agano la Kale na wakiwasihi wauamini kutubu kwa ajili ya dhambi za jamii yao, kana kwamba jamii ni kama Israel ya Agano la Kale. Tunapaswa kuendelea kuhubiri Injili ya Yesu Kristo hadi mwisho utakapotujia.
Watu wanapokea msamaha na wokovu ambao tayari Kristo amekwishaununua kwa ajili yao, pale wanaposikia na kuamini habari njema. Lakini kabla watu wenyewe hawajatubia dhambi zao na kusikia habari njema, maombi yetu wala toba haviwezi kumshawishi kusamehe dhambi hizo, au kuleta upatanisho kwa ajili yao au kwa ajili ya nchi yao. Kuyafikiria hayo au kuyatenda, huu ni ushirikina wa kidini na wala sio vinginevyo! Hayana msingi wowote katika neno la Mungu. Ni sawa, Mungu amewasamehe dhambi zao katika Kristo kwa sababu ya Kalvari, lakini hata kama ni hivyo, hiyo haileti manufaa yoyote katika maisha yao mpaka tu pale watakapotubu na kuaimini Injili.
Kwa hiyo, hebu basi kwa hakika tuombe, ili kwamba Mungu atume watenda kazi wake ili Neno la Mungu lipate kuletwa kwa waume kwa wake na kuwaongeza katika kanisa lake. Tuombe kwamba Mungu afungue mlango wa usemi kwa wale wadumuo kwa jina lake, kwamba Injili hiyo ipate kuifikia mioyo ya watu wengi na kuwarejesha kwa mwokozi.
Ni jambo moja la kuombea nalo ni kwamba Bwana wa mavuno apeleke watenda kazi katika mavuno yake (Luka 10:2); au kuwawezesha watumwa wake kuihubiri ile siri ya Injili kwa ujasiri (Efeso 6:19), au kwamba aweze kufanya maajabu kupitia watu wake ili wasioamini waweze kufikiwa (Mtd 4: 29,30); au kuhuzunishwa kwa sababu ya ugumu wa mioyo ya wale tunaowajua na wengineo pia na kwa hivyo kuomba ili kwamba Mungu aweze kuwaokoa (1 Tim 2:3,4; Rumi 9:1-3; 10:1); au kujinyenyekeza wenyewe na kuomba na kuombea katika kiti cha neema kwa ajili ya rehema ya Mungu iweze kuwafikia na kurejesha mioyo yao kwake pale ambapo wengine hutenda dhambi au kupotelea mbali (Gal. 4:19). Hayo yote ni mambo ambayo tunaweza na tunapaswa kuyafanya; lakini badala yake tunaona ni jambo la kinyume kabisa, pale tunapoanza kutubu kwa ajili ya dhambi za wenye dhambi na wakati huo huo kufikiri kuwa labda tunaweza kupokea msamaha na upatanisho kwa ajili yao na kwa nchi yetu pia!
Ni mchanganyiko wa kimawazo na upuuzi wa jinsi gani huu! Tumepotelea mbali kiasi gani na Biblia na mawazo yake. Kwanza, eti tuombe kwa jambo ambalo tayari Mungu amekwisha lifanya - kwa mfano, amewasamehe watu katika Kristo, na hii ameifanya bila malipo, bure - na kisha kujaribu tena na kusababisha msamaha huu ndani ya maisha yao kwa njia ya ujumla isiyofaa, kwa mfano, kwa kupitia maungamo na toba ya ushirikishwaji! Je, tunamjaribu Mungu kwa kulikataa neno lake na kupinga ukweli wake? Je, sio kwamba ni watu kwa makusudi kabisa ndio wanaoupinga ukweli wa Mungu lakini bila mashaka yoyote yale, hayo ni matokeo na mambo yaliyo sababishwa na mafundisho; pale wanapoongezea maombi yao ili kupata msamaha kwa ajili ya wenye dhambi.